NURU TUKUFU YA MTUME MUHAMMAD (s.a.w.w.)

1. Sheikh Shahabuddin Qastalani katika kitabu chake Mawahib al-Ladunniyyah ameandika hivi:- Alipokusudia Mwenyezi Mungu kuwaumba viumbe wake, aliichomoza Nuru ya Mtume Muhammad (s.a.w.w.); Nuru ambayo ni tukufu ndipo akaumba dunia.
Amehadithia Bwana Jabir bin Abdullah Ansari: “Nilipomwuliza Mtume Muhammad (s.a.w.w.) ‘Ya RASUL-ALLAHI wazee wangu nakufidia, nijulishe kiumbe yupi aliumbwa mwanzo?’. Akanijibu ‘Ewe Jabir, Mwenyezi Mungu aliumba nuru ya Mtume wake kutokana na nuru yake kabla ya kuumba chochote’”.

Na vile vile Sayyidna Ali (a.s.) ameeleza kwamba mpenzi wa Mwenyezi Mungu Mtume Muhammad (s.a.w.w.) amesema: “Mwenyezi Mungu ameumba nuru yangu miaka kumi na nne elfu kabla ya kumuumba Nabi Adam (a.s.)”.

2. Mwanahistoria maarufu wa Ki-Islamu Bwana Abul-Hasan Ali bin Husain al-Mas’udi katika kitabu chake maarufu cha historia kiitwacho Muruj adh-dhahab wa Ma’adin al-Jawahir, amepokea hadithi hii kutoka kwa Imam Ali (a.s.) kwamba Mwenyezi Mungu alipotaka kuumba dunia na watu na kila kilichomo ndani ya dunia, basi kwanza kabla ya kuiumba hii ardhi, kwa upekee kwa Nuru yake Jalali akaidhihirisha nuru yenye kung’aa kutokana na nuru yake na ikawa ile nuru inatoa cheche za nuru na mshabaha wa sura; tena akakusanya zile sura akaifanya sura moja na ikatokeza sura ya Mtume Muhammad (s.a.w.w.), basi hapo Mwenyezi Mungu akaikhutubia ile sura na kusema “Wewe ndiye niliyekuchagua, na wewe ndiye nuru yangu, kwako wewe nimewacha hazina ya uwongofu na kwa ajili yako (kwa mapenzi juu yako) mbingu nitainyanyua; na ardhi nitaitandaza na maji nitawacha yamiminike na yaende; na kujaalia thawabu na adhabu, Pepo na Jahannam (Moto) kwa watii na wasiotii; na nitawafanya Aali yako (AHLUL-BAYT) kuwa waongozi wa Haqi, na nitawajaza kwa elimu hata wasishindwe kueleza au kuwafahamisha Umma mushkili wowote wala jambo lolote lililofichika wasishindwe kulieleza, na nitawafanya wao (AHLUL-BAYT) wenye Hoja na Mfano juu ya viumbe wangu na kuwa nabihisha (kuwafahimisha  upekee/
Wahdaaniyah) wangu na Qudra yangu juu ya viumbe vyote”. Baadaye Mwenyezi Mungu akachukuwa Ahadi kwa kuyakubali yote, na kabla hakuchukua hiyo Ahadi akawajulisha viumbe vyote kwa kumchagua Mtume Muhammad (s.a.w.w.) na Aali zake kuwa ni waongozi wa Haqi na wamechaguliwa naye ili iwe ndio njia ya uadilifu na viumbe wasiwe na udhuru wowote wa kwamba hawakujua.


3. Bwana Abul Qasim al-Tabarani (360 A.H.) katika kitabu chake Muj’am al-Kabeer anahadithia kutokana na Bwana Ibn Abbas kwamba Mtume (s.a.w.w.) amesema: “Mimi nilikuwa Mtume wakati Adam (a.s.) alipokuwa kati ya roho na kiwiliwili (maana yake bado umbo la Nabi Adam lilikuwa halijakamilika)”.

Comments