UMUHIMU WA KUSOMA HISTORIA YA UISLAMU

Hamna shaka kuwa historia ya mwanadamu ndio chemchemu na chanzo cha maarifa, chanzo ambacho mataifa yanakihitaji katika safari yake yenye kuendelea. Na ndio chanzo pekee chenye uwezo wa kuhuisha na kulisukuma taifa mbele na kulipa sifa na hadhi maalum huku kikilifunganisha taifa hilo na mizizi yake ya ustaarabu ambayo hulizuwia taifa dhidi ya mmong'onyoko.

Qur'ani imemhimiza kila mwanadamu, ikamtaka azame ndani ya Historia ya mwanadamu na azingatie yaliyomo ili awaidhike na kuongoka, hivyo Mwenyezi Mungu akasema: "Je, hawatembei katika ardhi ili wapate nyoyo za kufahamia au masikio ya kusikilizia?"1.
 Baada ya Mwenyezi Mungu kutoa historia ya Adi, Thamudi, Firauni, watu wa miji iliyopinduliwa na watu wa Nuh akasema: "Ili tuifanye ukumbusho kwenu na sikio lisikialo lisikie."2
Historia ya ujumbe mbalimbali wa Mwenyezi Mungu imejaa masomo na mazingatio, masomo ambayo yameonyesha jinsi manabii watukufu walivyojali mataifa yao ili kuyaokoa toka kwenye matatizo mbalimbali.

Pia ujumbe huo umeonyesha lengo na mwelekeo wake wenye kujaa nuru na manufaa. Kwa ajili hiyo sira ya Mtukufu Mtume (s.a.w.w.) na kizazi chake huwa ni tafsiri ya kivitendo ya misingi na sheria za kiislamu.

Hivyo kusoma sira yao na historia ya maisha yao ni chanzo muhimu cha kuifahamu Qur'ani na Sunna, na ni chemchemu ya maarifa ya wanadamu wote, kwa sababu ni ujumbe wa Mwenyezi Mungu alioutuma kwa wanadamu kupitia kwa Nabii wa mwisho na mawasii wake wateule wakiwa ni viongozi wa wanadamu wote bila kubagua.

Kwa kuwa umma wote umekubaliana juu ya wema na utakaso wa viongozi wa ujumbe wa Mwenyezi Mungu basi inafaa kuwafundisha watu historia ya maisha yao ndani, kwani Qur’ani imetamka wazi kuhusu umaasumu na utakaso wao ili wawe ni kiigizo chema kwa yule anayetarajia fadhila za Mwenyezi Mungu na malipo mema ya Siku ya Kiyama.
Rejea
1. Al-Hajj: 46.

2. Al-Haaqah: 12.

Comments