Kwa nini nisijute; bali ni kwa nini kila
Muislamu asijute wakati usemwapo ukweli huu unaoelezea hasara waliyoipata
Waislamu kutokana na kutengwa kwa Imam Ali kwenye Ukhalifa ambao Mtume wa
Mwenyezi Mungu alimtawalisha, na hivyo kuunyima umma (wa Kiislamu) uongozi wake
na hekima, na elimu yake nyingi.
Na pindi Muislamu atakapochunguza bila ya chuki
wala upendeleo, atamkuta Imam Ali ndiyo mwenye elimu na mjuzi mno kuliko watu
wote baada ya Mtume (s.a.w), kwani tunashuhudia historia inayotuonesha kwamba
wanachuoni wa Kisahaba walikuwa wakimuuliza Ali kwa kila lililowatatiza, na
kauli ya Umar bin Al-Khatab aliyoisema zaidi ya mara sabini ya kwamba "Lau
kama si Ali basi Umar angeliangamia' لولا علي لهلك عمر wakati ambapo Imam Ali (a.s.) hakupata kamwe
kumuuliza Sahaba yeyote miongoni mwao.
Kama ambavyo historia inakiri kuwa Ali bin Abi
Talib ni shujaa mno na mwenye nguvu kuliko Masahaba wote, na kuna mashujaa
wengi miongoni mwa Masahaba waliokimbia vita katika sehemu nyingi tu, wakati
ambapo Imam Ali (a.s.) alisimama imara mahala pote palipopiganwa vita, na
inatosha kuwa ni dalili ile nishani aliyopewa na Mwenyezi Mungu pale Mtume
(s.a.w.w) aliposema:
"Kesho nitampa bendera yangu mtu
anayempenda Mwenyezi Mungu na Mtume wake, naye anapendwa na Mwenyezi Mungu na
Mtume wake, mkali katika mapambano si mwenye kukimbia, Mwenyezi Mungu amekwisha
unawirisha moyo wake kwa imani".
Masahaba wakaitamania (kuipata) bendera hiyo,
Mtume akampa Ali bin Abi Talib.
Kwa kifupi, bila ya shaka maudhui ya elimu ,
nguvu na ushujaa, ni sifa ambazo Imam Ali alikuwa nazo, ni maudhui
yanayofahamika kwa wote (Sunni na Shia) na ukiachilia mbali maandiko
yanayojulisha kwa uwazi wa kuashiria juu ya Uimamu wa Ali, hapana shaka kwamba
Qur'an haikubali uongozi na Uimamu isipokuwa kwa mtu mwenye elimu, shujaa tena
mwenye nguvu.
Mwenyezi Mungu anasema kuhusu wajibu wa
kuwafuata wanachuoni (wenye elimu). pale Allah (s.w) aliposema:-
قُلْ هَلْ مِن شُرَكَآئِكُم مَّن يَهْدِى إِلَي الْحَقِّ قُلِ اللّهُ يَهْدِى لِلْحَقِّ اَفَمَن يَهْدِى إِلَي الْحَقِّ اَحَقُّ اَن يُتَّبَعَ اَمَّن لاَّ يَهِدِّى إِلاَّ اَن يُهْدَي فَمَا لَكُمْ كَيْفَ تَحْكُمُونَ[1]
Sema: Je! Yupo katika miungu yenu ya ushirikina
anaye ongoa kwendea Haki? Sema: Mwenyezi Mungu anaongoa kwendea Haki. Basi, je,
anaye stahiki kufuatwa ni yule Mwenye kuongoa kwendea Haki au asiye ongoa ila
aongozwe yeye? Basi nyinyi mna nini? Mnahukumu namna gani?).
Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu kuhusu wajibu
wa kumfuata mwenye elimu, shujaa tena mwenye nguvu:
وَقَالَ لَهُمْ
نَبِيُّهُمْ إِنَّ اللّهَ قَدْ بَعَثَ لَكُمْ طَالُوتَ مَلِكاً قَالُوَاْ اَنَّي
يَكُونُ لَهُ الْمُلْكُ عَلَيْنَا وَنَحْنُ اَحَقُّ بِالْمُلْكِ مِنْهُ وَلَمْ
يُؤْتَ سَعَةً مِّنَ الْمَالِ قَالَ إِنَّ اللّهَ اصْطَفَاهُ عَلَيْكُمْ وَزَادَهُ
بَسْطَةً فِى الْعِلْمِ وَالْجِسْمِ وَاللّهُ يُؤْتِى مُلْكَهُ مَن يَشَاءُ
وَاللّهُ وَاسِعٌ عَلِيمٌ[2]
Na Nabii wao akawaambia: “Mwenyezi Mungu
amekuteulieni Taluti (Sauli) kuwa ni mfalme. Wakasema: vipi atakuwa na ufalme
juu yetu, na hali sisi tuna haki zaidi kupata ufalme kuliko yeye, naye hakupewa
wasaa wa mali? Akasema: Mwenyezi
Mungu amemteua yeye juu yenu na amemzidishia ukunjufu wa ilimu na kiwiliwili.
Na Mwenyezi Mungu humpa ufalme wake amtakaye. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye wasaa
na Mjuzi”.
"Wakasema, ni vipi atakuwa na ufalme juu
yetu, na hali sisi tunastahiki zaidi kupata ufalme kuliko yeye, naye hakupewa
wasaa wa mali? Akasema, Mwenyezi
Mungu amemchagua juu yenu na amemzidishia wasaa wa elimu na kiwiliwili na
Mwenyezi Mungu humpa ufalme wake amtakaye, naye Mwenyezi Mungu ni mwenye wasaa
mwenye kujua".
Hapana shaka Mwenyezi Mungu Mtukufu amemzidishia
Imam Ali wasaa wa elimu kuliko Masahaba wote, akastahiki kuwa ni "Mlango
wa elimu," pale Mtume Muhammad (s.a.w.w) aliposema aliposema:-
“ انا مدينة العلم وعلي بابها"
akawa ndiye rejea pekee kwa Masahaba baada ya
kufariki Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) nao Masahaba walikuwa kila
wanaposhindwa kutatua mambo husema "Mas-ala haya magumu hakuna ayawezaye
isipokuwa Imamu Aliy (a.s) ."
Na alimzidishia wasaa wa kiwiliwili, kwa kweli
alistahiki kuwa simba wa Mwenyezi Mungu aliye mshindi, na nguvu zake na ushujaa
wake ni wenye kupigiwa mfano katika kila zama kiasi kwamba wanahistoria
wamesimulia visa vingi kuhusu ushujaa na nguvu zake visa ambavyo vinakurubia
kuwa ni miujiza, kama vile kuung'oa mlango wa Khaybar, wakati ambapo Masahaba
ishirini walishindwa hata kuutikisa. Na pia kuling'oa Sanamu kubwa la Hubal.
kutoka juu ya paa la Al-Kaabah na kulisogeza jiwe kubwa ambalo jeshi lote
lilishindwa hata kulitikisa, na mengineyo miongoni mwa riwaya mashuhuri.
Na Mtume (s.a.w.w) alimsifu na kumtaja kwa ubora mwana wa ammi yake Ali, na akazibainisha fadhila zake mahala mbali mbali na aliyatambulisha mambo yake maalum yanayomuhusu na daraja yake.
Kuna wakati Mtume akisema:
"Hakika huyu ni ndugu yangu na ni wasii
wangu na ni Khalifa wangu baada yangu, basi msikilizeni na mumtii"
Na kuna wakati Mtume humwambia Ali (a.s.):
"Wewe kwangu mimi unayo daraja ya Harun kwa
Musa isipokuwa hapana Nabii baada yangu".
Na kuna wakati mwingine Mtume akisema:
"Yeyote mwenye kutaka kuishi nilivyoishi
mimi na kufa mauti (kama) yangu na akae katika bustani ya milele aliyoniahidi
Mola wangu, basi na amtawalishe Ali bin Abi Talib, kwani yeye hatakutoeni
kwenye uongofu na kamwe hatakuingizeni katika upotofu".
Na yeyote atakayefuatilia sera ya Mtume Mtukufu
(s.a.w.w) atamkuta Mtume hakutosheka kwa kusema maneno tu na hadithi
zinazomuhusu Ali, bali maneno yake yakionekana kwa matendo yake, kwani katika
uhai wake Mtume katika uhai wake hakupata kumuwekea Ali amiri yeyote juu yake
miongoni mwa Masahaba pamoja na kwamba alikuwa akiwawekea maamiri Masahaba
wengine wao kwa wao. Hapana shaka kwamba Mtume aliwawekea Abubakar na Umar
amiri (wa kuwaongoza) katika vita ya "Dhatus-Salasil" amiri huyo
alikuwa Amr bin Al-As .
Kama ambavyo Mtume (s.a.w.w) aliwawekea Masahaba
amiri ambaye alikuwa kijana mdogo Usamah bin Zaid na hilo alilifanya katika jeshi la Usamah kabla ya kufariki kwake yeye
Mtume (s.a.w.w.).
Amma Ali bin Abi Talib hakuwa katika ujumbe
wowote ila yeye ndiye amiri, hata kuna wakati fulani Mtume (s.a.w.w.) alituma
ujumbe wa namna mbili, akampa uamiri Ali kwenye moja ya ujumbe huo na Khalid
bin Walid akampa uamiri kwenye ule wa pili kisha akawaambia:
"Mutakapoachana kila mmoja awe amiri wa
jeshi lake na mkikutana basi Ali ndiye
amiri wa jeshi lote.”
Kutokana na maelezo yote yaliyotangulia tunakuta
kwamba Ali ndiye mtawalia mambo ya waumini baada ya Mtume (s.a.w.w.) na haifai
kwa yeyote yule kumtangulia.
Lakini kwa masikitiko makubwa, Waislamu wamepata
hasara kubwa, na ndiyo maana wanapata taabu hadi leo na wanachuma matunda ya
kile walichokipanda, na bila shaka waliokuja baadaye wamekwisha yatambua yale
yaliyoasisiwa na hao waliotangulia.
Hivi kweli inawezekana kwa mtu yeyote kufikiria
kuna Ukhalifa ulioongoka zaidi ya ule Ukhalifa wa Ali bin Abi Talib? Lau umma
huu ungelifuata kile alichokichagua Mwenyezi Mungu na Mtume wake, kwa kuwa Ali
alikuwa ndiye mwenye uwezo wa kuuongoza umma (huu) kwa muda wote wa miaka
thelathini juu ya mfumo mmoja kama vile alivyouongoza Mtume wa Mwenyezi Mungu
(s.a.w.w) bila ya mabadiliko yoyote. Tunasema hayo kwa kuwa Abu Bakar na Umar
walibadilisha na wakafanya ijtihadi zao dhidi ya maagizo na matendo yao yakawa ndiyo sunna inayofuatwa. Othman naye alipokuja kwenye
Ukhalifa akabadilisha mengi mno mpaka ikasemwa kuwa alikikhalifu kitabu cha
Mwenyezi Mungu na Sunna ya Mtume wake pia Sunna ya Abubakar na Umar, hapo ndipo
Masahaba walipompinga na yakafanyika dhidi yake mapinduzi makubwa
yaliyoangamiza Maisha yake na kusababisha fitna kubwa katika umma (fitna
ambayo) jeraha lake halijapona hadi leo.
Ama Ali bin Abi Talib, yeye alikuwa akifungamana
na Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunna ya Mtume wake, hakwenda kinyume na yale
anayoyaridhia Mwenyeezi Mungu, na ushahidi mkubwa wa hilo ni kwamba yeye Imam
Ali alikataa kuchukua Ukhalifa pale walipomuwekea sharti ya kuhukumu kwa kitabu
cha Mwenyezi Mungu na sunna ya Mtume wake na sunna ya Makhalifa wawili
waliomtangulia.
Huenda akauliza muulizaji: Basi ni kwa nini Ali
anashikamana na kitabu cha Mwenyezi Mungu na sunna ya Mtume wake wakati ambapo
Abubakar na Umar na Uthman walilazimika kufanya ijtihadi na mabadiliko?
Jawabu ni kuwa, yeye Ali anayo elimu ambayo wao
hao hawakuwa nayo, isitoshe Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) alimuhusisha kwa
milango elfu moja ya elimu na katika kila mlango anaweza kufungua milango elfu
moja.
Pia alimwambia: "Wewe Ewe Ali utaubainishia
umma wangu yale watakayotofautiana ndani yake baada yangu. "
Amma hao Makhalifa walikuwa hawajuwi mambo mengi
katika hukmu za Qur'an za dhahiri licha ya taawili ya Qur'an, hali hii
wamethibitisha Bukhar na Muslim ndani ya sahih zao katika mlango wa kutayamamu
ya kwamba, kuna mtu fulani alimuuliza Ummar bin Al-Khatab katika zama za
Ukhalifa wake akasema yule mtu: "Ewe Amirul-Muuminina hakika mimi
nimepatwa na janaba na sikupata maji, basi nifanyeje"? Umar akasema:
"Usiswali"!! Kadhalika Umar hakuifahamu hukmu ya watoto wa ndugu wa
kiume wa baba (ibnu Ammi) mpaka amekufa na hali ya kuwa anasema, "Natamani
lau ningemuuliza Mtume wa Mwenyezi Mungu juu ya watoto wa Ammi".Wakati
ambapo hukmu yake imetajwa ndani ya Qur'ani Tukufu, kwa hiyo Umar ambaye
Masunni wanasema kuwa alikuwa miongoni mwa wenye kupewa Il-hamu (na Mwenyezi
Mungu) hali ya elimu yake ilikuwa katika kiwango hiki, (basi kama Umar ni hivi)
hao wengine wala usijisumbue kuuliza, hao ndiyo ambao waliingiza Bid'a (uzushi)
ndani ya dini ya Mwenyezi Mungu bila ya kuwa na elimu wala uongofu wala kitabu
cha kuwaongoza isipokuwa jitihada zao binafsi.
Na huenda msemaji akasema: "Ikiwa mambo
ndiyo yako namna hii, basi ni kwa nini Imam Ali (a.s.) hakuubainishia umma yale
ambayo walitofautiana ndani yake baada ya Mtume (s.a.w.w)"
Jawabu ni kuwa: Imam Ali (a.s.) hakuacha kufanya
juhudi katika kubainisha yale yaliyoutatiza umma, na yeye alikuwa ndiye marejeo
ya Masahaba kwa kila lililowatatiza alikuwa akija na kufafanua na kutoa nasaha.
Hivyo basi walikuwa wakiyachukua yale wayapendayo na yasiyopingana na siasa zao
na kuyaacha yasiyokuwa hayo, na historia ndiye shahidi mkubwa kwa haya
tuyasemayo.
Kwa kweli lau siyo Ali bin Abi Talib na Maimamu
miongoni mwa wanawe, basi watu wasingeyafahamu mafunzo ya dini yao, lakini watu
(walivyo) ni kama ilivyotufunza Qur'an yakuwa hawaipendi haki, basi walifuata
matamanio yao na kuzusha madhehebu dhidi ya Maimamu wa nyumba ya Mtume ambao
serikali zilizokuwa katika wakati wao zilikuwa zikifuatilia kila wasemalo, wala
hazikuwapa uhuru wa kushughulika na kufanya mahusiano ya moja kwa moja na watu.
Basi Imam Ali (a.s.) alikuwa akipanda juu ya
mimbari na kuwaambia watu, "Niulizeni kabla hamjanikosa" Na yatosha
kuwa Imam Ali ameacha Nahjul-Balagha, nao Maimam kutoka katika nyumba ya Mtume
(s.a.w.w) wameacha elimu ambayo imeenea ulimwenguni na hilo wamelishuhudia viongozi wa Kiislamu Masunni na Mashia.
Sasa tunarudia kwenye maudhui na kusema:
"Kwa msingi huu, lau Ali angewezeshwa kuuongoza umma kwa miaka thelathini
kwa mujibu wa sera ya Mtume (s.a.w.) basi Uislamu ungeenea na kuimarisha
itikadi katika nyoyo za watu zaidi na kwa undani wala pasingekuwa na fitna
ndogo au kubwa wala (mauaji ya) Karbala yasingekuwepo wala msiba wa Ashuraa.
Lau tutaukadiria uongozi wa Maimamu kumi na moja baada ya Ali, Maimamu ambao
Mtume wa Mwenyezi Mungu aliwataja, na uhai wao uliendelea kwa kipindi cha karne
tatu, basi pasingebaki hapa duniani miji isiyokuwa ya Kiislamu, na ulimwengu
usingekuwa katika hali tunayoishuhudia leo hii na maisha yetu yangekuwa ya
kibinaadamu kwa maana yake ya hakika lakini Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema:
"[3]الم, اَحَسِبَ النَّاسُ اَن يُتْرَكُوا اَن
يَقُولُوا آمَنَّا وَهُمْ لاَ يُفْتَنُونَ"
"Alif Lam Mim, Je, watu wanadhani kwamba
wataachwa kwa kuwa wanasema: "Tumeamini" wasijaribiwe (wakapata
Mitihani)? Umma wa Kiislamu umefeli katika mtihani huu kama vile zilivyofeli
umma zilizotangulia, kama ambavyo Mtume wa Mwenyezi Mungu, alivyotamka katika
minasaba mbali mbali na kamaambavyo Qur'an
ilivyosisitiza mara nyingi ndani ya aya nyingi.
[1] Surat Yunus Aya ya 35
[2] Suratul-Baqarah Aya ya
247
[3] Surat Ankabuut Aya ya 2
Comments
Post a Comment