HISTORIA NA SIRA ZA VIONGOZI WAONGOFU(UTANGULIZI)

Qur'ani imemhimiza kila mwanadamu ikamtaka azame ndani ya historia ya mwanadamu na azingatie yaliyomo ili awaidhike na kuongoka, hivyo Mwenyezi Mungu akasema: "Je, hawatembei katika ardhi ili wapate nyoyo za kufahamia au masikio ya kusikilizia?"1

Baada ya Mwenyezi Mungu kutoa historia ya Adi, Thamudi, Firauni, watu wa miji iliyopinduliwa na watu wa Nuh akasema: "Ili tuifanye ukumbusho kwenu na sikio lisikialo lisikie."2. Historia ya ujumbe mbalimbali wa Mwenyezi Mungu imejaa masomo na mazingatio, masomo ambayo yameonyesha jinsi manabii watukufu walivyojali mataifa yao ili kuyaokoa toka kwenye matatizo mbalimbali.

Pia ujumbe huo umeonyesha lengo na mwelekeo wake wenye kujaa nuru na manufaa. Kwa ajili hiyo sira ya Mtukufu Mtume (s.a.w.w.) na kizazi chake huwa ni tafsiri ya kivitendo ya misingi na sheria za kiislamu.
Hivyo kusoma sera yao na historia ya maisha yao ni chanzo muhimu cha kuifahamu Qur'an na Sunna, na ni chemchemu ya maarifa ya wanadamu wote, kwa sababu ni ujumbe wa Mwenyezi Mungu alioutuma kwa wanadamu huku Nabii wa mwisho na mawasii wake wateule wakiwa ni viongozi wa wanadamu wote bila kubagua.


Kwa misingi hii nitaendelea kuleta mada hatua kwa hatua kuhusu sira ya viongozi hawa watukufu ili tuitumie kama mwongozo wa kuitafsiria Qur’an na hivyo kupata mwongozo kamilifu katika maisha yetu ya kiuchamungu. 

Comments