Amenakili Sheikh As-Sadduq r.a. kutoka kwa Al Imam
'Ali ar-Ridha (a.s.) kutokea kwa Al Imam Musa al-Kadhim a.s. kutokea kwa Al
Imam Ja'afer as-Sadiq a.s. kutokea kwa Al Imam Muhammad al-Baqir a.s. kutokea
Al Imam Zaynul 'Aabediin a.s. kutokea kwa Al Imam Hussein ibn ‘Ali ibn Abi
Talib a.s. kutokea Imam Amir Al-Muuminiin Al Imam ‘Ali ibn Abi Talib a.s.
kutokea kwa Mtume Muhammad Mustafa (s.a.w.w.):
“Ya ayyuha-Naas (Enyi watu)! Kwa hakika Mwezi wa Allah (sw)
umewafikieni pamoja na baraka, rehema na misamaha yake, kwani ni mwezi ulio
bora kwa Allah (sw), usiku na mchana wake ni bora kuliko usiku na mchana wowote
mwingine, saa zake ndizo bora kabisa kuliko saa zote na ni mwezi ambamo Allah (sw)
anakualikeni na kuwafanyeni katika watu waliokirimiwa, pumzi zenu katika Mwezi
huu ni Tasbihi, na usingizi wenu humo ni ‘
ibada, na ‘amali zenu humo zinakubaliwa na Dua’a zenu
humo zinajibiwa na hivyo mumwombe Allah (sw) kwa nia safi na iliyo kweli na
moyo msafi ili awajaalieni tawfiqi ya kufunga saumu na usomaji wa Qur’ani
Tukufu katika mwezi huu mtukufu. Kwa hakika yeyote atakayekosa msamehe wa Allah
(sw) katika mwezi huu ulio Adhimu basi atakuwa ni mtu asiyebahatika.
Mkumbukeni njaa na kiu cha Siku ya Qiyamah mkiwa
katika hali ya njaa na kiu katika mwezi huu mtukufu, na vile vile, mutoe sadaqa
zenu kwa ajili ya mafukara na masikini miongoni mwenu, muwaheshimu walio
wakubwa wenu, na kuwahurumia walio wadogo miongoni mwenu na muwajaze kwa huruma
zenu.
Mzihifadhi ndimi zenu na muyaweke macho yenu chini kwa
yale yote yasiyoruhusiwa kutazamwa na wala msiyasikie yale yote yasiyoruhusiwa
kusikilizwa, muwawie vyema mayatima ili wanapokuwa watoto wenu mayatima, nao
pia watendewe mema na mumwombe Allah (sw) msamaha wa madhambi yenu, na
mnyoosheeni Allah (sw) mikono yenu kwake kwa ajili ya Dua’a katika nyakati za
Sala kwani ndiyo iliyo saa bora kabisa
ambamo Allah (sw) huwatazama wanaomwabudu kwa Rehema
na hujibu anapoombwa na huitikia anapoitwa.
Ya ayyuha-Naas (Enyi watu)! Kwa hakika nafsi zenu zinategemea amali zenu na muzikomboe kwa
istighfar zenu, migongo yenu imelemewa kwa uzito wa madhambi yenu na hivyo mpunguze
uzito wenu kwa kurefusha sijida zenu na mjue kuwa Allah (sw) ametamka kwa kula
kiapo cha Ukuu Wake kwa kutowaadhibu wanaosali na wanaosujudu na kutowatishia
moto Siku ya Qiyamah, ambamo watu watakuwa wamesimama mbele ya Mola wao.
Ya ayyuha-Naas (Enyi watu)! Miongoni mwenu atakayemfuturisha aliyefunga saumu katika funga za Mwezi
huu Mtukufu basi ni sawa na kupata thawabu za kumpatia
uhuru mtumwa mmoja na kupatiwa msamaha wa madhambi yaliyopita.”
Masahaba walisema: “Ewe Mtume Mtukufu (s.a.w.w.)! Si
wote tulio na uwezo huo.” Mtume Muhammad Mustafa
(s.a.w.w.) alijibu: “Jiepusheni na moto wa Jahannam
hata kwa kulisha kipande cha tende au hata kwa kunywisha maji. Kwa hakika Allah
(sw) hupendezewa na hulipa mema kwa atendaye hivyo hata kama hatakuwa na zaidi.
”
Ya ayyuha-Naas (Enyi watu)! Yeyote atakayezirekebisha tabia zake basi Allah (sw) atamfanyia
wepesi upitishio wake siku ya Qiyamah juu ya Siraat ambapo miguu ya wengineo
ikitetemeka, na yeyote yule atakayewafanyisha kazi kidogo wamfanyakazi wake
siku hizi za funga, basi Allah (sw) pia atamfanyia wepesi
hesabu yake Siku ya Qiyamah, na yeyote yule
atakayeziepusha shari zake kwa watu, basi Allah (sw) atamwepusha na ghadhabu
Zake, na yeyote atakayewakirimu mayatima basi Allah (sw) atamkirimu Siku ya Qiyamah
na yeyote atakayewatendea mema ndugu na jamaa zake basi Allah (sw) atamjaalia
Rehema Zake Siku ya Qiyamah.
Na yeyote atakayevunja uhusiano wake pamoja na jamaa
na ndugu zake, basi Allah (sw) pia atauvunja uhusiano wake pamoja mtu huyo. Na
atakayesali Sala za Sunnah katika mwezi huu Mtukufu, basi Allah (sw)
atamwepusha na adhabu za Kaburi.
Comments
Post a Comment