NJIA ZA KUTUMIA ZAKA

NJIA ZA KUTUMIA ZAKA
Kurani Tukufu imetaja njia nane za kutumia Zaka:
(1) Kuwapa mafukara, watu ambao umaskini wao umeonekana waziwazi:
(2) Maskini, ambao wameishiwa mali au njia za kuchumia mali lakini wanajaribu kuuficha umaskini wao wasiudhihirishe kwa wengine kwa sababu ya ari ya moyo wao;
(3) Wafanyao kazi ya kukusanya Zaka,
(4) Waungiwao mioyo yao, yaani watu ambao nyoyo zao zimeelekea kwenye dini, lakini kwa kuwa wametengana na jamaa zao, wanakuwa na haja ya msaada. Hiyo siyo maana yake kwamba watu wapewe fedha na kuvutwa kuingia dini ya Islamu, bali watu wapya katika dini ambao pengine wanaachishwa kazi au wanataabishwa kwa njia nyinginezo kwa sababu ya wao kuacha dini yao ya zamani na kukubali dini ya Islamu wamewekewa sehemu katika mali ya Waislamu.
(5) Kuwakomboa wafungwa na watumwa. Wale watu ambao wanafungwa kwa kutoweza kulipa deni pia wanaweza kusaidiwa na pesa hizo. Hata wafungwa na watumwa wasiokuwa Waislamu wanaweza kukombolewa na kuachwa huru kwa fedha ya Zaka
(6) Wasio na uwezo wa kulipa madeni yao au walipata hasara; nzito katika biashara zao au waliotakiwa kulipa dia (fidia kwa mtu aliyefariki) ya jamaa zao;
(7) Katika njia ya Mwenyezi Mungu: katika fungu hili yanaingia matumizi yote yanayofanywa kwa ajili ya dini ya Mwenyezi Mungu au kwa ajili ya watu wote kwa jumla; kama kueneza na kupigisha chapa vitabu na magazeti ya dini, kufungua shule za elimu za dini na za kidunia, kuendesha hospitali na viwanda vya sanaa na mambo mengine yote yenye kustawisha Waislamu na dini yao; (8) Wasafiri wanaopata taabu katika safari kwa kupungukiwa pesa au wanaosafiri kutafuta elimu. Msafiri ye yote awe tajiri au maskini anaingia katika fungu hili. Nyumba za wageni zaweza kujengwa kwa fedha ya Zaka. Wasio Waislamu pia wanaweza kualikwa waje watembelee nchi za Waislamu na kuonana nao wakalipwa kwa fedha ile.
Matumizi ya Zaka yana wasaa mwingi na watu wote wanapata faida. Siku za Khalifa wa Kiislamu, yaani Imam Ally (a.s) Mayahudi na maskini wengine wa dini zingine walikuwa wakipata msaada mwezi hata mwezi katika beit-il-mal ya Waislamu. Watu walioshindwa kujipatia riziki kwa sababu ya uzee au ugonjwa au kwa kukosa njia za kuchumia mali walisaidiwa na Maimamu wa Mtume s.a.w. kwa njia ya Zaka na Khumsi.

Lakini watawala waliovamia utawala baada tu ya Mtume kufariki, waliwanyima familia ya Mtume (s.a.w.w) haki yao ya khumsi ambayo walikuwa wamepewa na Allah (s.w). Waliwanyima Mali hizo ili kuwadhoofisha na kiuchumi, waweze kuzitii tawala zao za kidhalimu. 

Comments