UIMAMU (UKHALIFA)

UIMAMU (UKHALIFA)
Msimamo wa Aya zilizokuja juu ya uongozi ukisoma yalioandikwa katika vitabu mbali mbali na Hadithi zilizothibiti, na tarikh inayoonyesha katika jambo hili, utapata mambo makuu matatu ambayo yanaonyesha kuwa:
Uimamu/Ukhalifa lazima uteuliwe na Mwenyezi Mungu. Na kwa upande wa pili utaona kuwa Nyimati zilizopita zilifuata uongozi uliochaguliwa na Mwenyezi Mungu, wala jambo hilo halikuachiwa watu wenyewe kwa njia ya kuchaguwana.
Jambo la kwanza lililoongoza baina ya Mitume waliopita ilikuwa ni kusalimu amri na kufuata uongozi wa Mwenyezi Mungu, na kila alipoondoka Mtume aliweka atakaeshika nafasi yake. Wengi wao waliorithi kazi zao walikuwa Manabii, hata hivyo baadhi yao hawakuwa Manabii bali walikuwa Mawasii tu.
Jambo la pili: Uongozi katika nyimati zilizopita ulipatikana kwa njia ya kurithi baina ya vizazi katika koo za Mitume kama tunavyosoma katika Aya zifuatazo: a. "Hakika Mwenyezi Mungu alimchagua Adam na Nuh na Kizazi cha Ibrahim na Kizazi cha Imrani juu ya walimwengu wote. Ni kizazi cha wao kwa wao, na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia Mwenye kujua" 3:33-34
b. "Na tulimpa Isihaqa na Yaaquubu na tukaweka katika Kizazi chake Unabii na Kitabu, na tukampa ujira wake katika dunia. Nae katika akhera kwa hakika atakuwa miongoni mwa watu wema." 29:27
c. "Na hakika tulimpeleka Nuhu na Ibrahim na tukauweka katika kizazi chao Unabii na kitabu." 57:26

d. Mwenyezi Mungu alimweka Ibrahim kuwa Imam (Kiongozi wa watu). Ibrahim alimuomba Mola wake awape nafasi hiyo vile vile katika kizazi chake. Mwenyezi Mungu hakumkemea wala kumgombeza, ila alimwambia ya kuwa: "Haiwafakii ahadi yangu (Unabii and Uimam) watu madhalimu." 2:124.
e. Nabii Musa (a.s.) alipoomba kwa Mwenyezi Mungu ndugu yake Haruna awe msaidizi wake katika uongozi, Mwenyezi Mungu hakumkasirikia wala kumkatalia ombi hilo. "Na unijaalie waziri katika jamaa zangu, Haruna ndugu yangu. Uniimarishe kwake nguvu zangu, na umshirikishe katika kazi yangu. Ili tukutukuze sana, na tukutaje kwa wingi. Hakika wewe unatuona, akasema hakika umepewa maombi yako ewe Musa" 20:29-36.
Musa alimweka Haruna kuwa Khalifa wake alipoondoka, kama Quran inavyosema: "Na tulimwahidi Musa siku thelathini na tukatimiza kwa kumi ikatimia miadi ya Mola wake siku arobaini. Na Musa akamwambia ndugu yake Haruna: Shika mahala pangu katika watu wangu na usuluhishe wala usifuate njia ya waharibifu." 7:142 Katika Aya hizi tumeona nafasi ya Uongozi inavyoendelea kati ya Kizazi na Kizazi baina ya koo za Manabii.

Utaratibu ni huu wa mtume kuweka mrithi wake katika uongozi, na ndivyo Mtume Muhammad (s.a.w.w) alimteua imam Ally (a.s) kuongoza umma wakati atakapofariki dunia. Lakini wababe wakapinga na kuchukua madaraka kwa nguvu. Na huo ndio mwanzo wa mgawanyiko kwa waislamu. Waliafikiana na Mtume juu ya ukhalifa kuwa wa Imam Ally huitwa Mashia na wale waliopinga na kuamua kuchaguana na ndipo Abubakar alipochaguliwa hutwa Ahlulsunnah waljamaa. 

Comments