ZAKAT NI HAKI YA MASKINI

Juu ya sadaka hii Mtume (s.a.w.) alisema kuwa “Zaka inachukuliwa kwa matajiri wa Waislamu na hurudishiwa mafukara wao”.
Neno la "kurudishiwa" linastahili kufikiriwa kidogo. Mtume (s.a.w.w) hakusema "hupewa" bali alisema "hurudishiwa". Mradi wake ni kwamba watu wanaopewa sehemu katika Zaka
hawafanyiwi hisani na wenye kuitoa, bali kwa hakika wanapokea haki yao.

Kurani Tukufu imesema. "Na Amekutiishieni vilivyomo mbinguni na vilivyomo ardhini vyote vimetoka Kwake" (45:14).
Tena amesema, "Na ambao katika mali zao iko sehemu maalumu kwa ajili ya aombaye na
anayezuilika kuomba" (70:25,26): Basi mtu anayechuma mali, hiyo yote si yake peke yake;
bali iko ndani yake haki ya watu wengine. Kwa maana ardhi na mvua na wanyama na madini na vyombo vingine vya kuchumia mali, kwa hakika, viliumbwa kwa ajili ya wanadamu wote.
Basi tajiri anayechuma mali kwa kutumia vile vitu vilivyoumbwa si kwa ajili yake tu awe na

hakika ya kuwa haki ya watu wengine haikosi kuwamo katika mali yake. Na asipotoa haki ya watu hao mali yale hayatakuwa halali kwake. Ndiyo sababu neno lililotumiwa kwa sadaka hiyo ni "zaka", yaani kitu cha kutakasa mali. Kwa maneno mengine, mali aliyopata mtu haiwi halali kwake mpaka awe ametoa sehemu maalumu kwa ajili ya watu wengine ambayo ni haki yao.

Comments