JUA LAREJESHWA KWA AJILI YA IMAM ALLY (a.s)

JUA LAREJESHWA KWA AJILI YA IMAM ALLY (a.s)
Imeelezwa katika Marijun Nubuwah kwamba aliporejea Mtume (s.a.w.w) kutoka Khaibar alipofika kwenye kituo “Sahba” baada ya kuswali sala ya alasiri, Mtume akaweka kichwa chake kwenye miguu ya Ali (a.s) na akalala.
Katika hali ya kulalal hali ya kutemshwa wahyi ikadhihiri kwake na ikaendelea mpaka jua likazama. Ali (a.s) alikuwa hajaswali swalatil asri. Ulipokwisha kushuka wahyi Mtume akamuuliza, Ali umeswali sala ya alasiri? Imam Ali akajibu sikuswali, ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu. Mtume akaomba kwa Mwenyezi Mungu, ‘ewe Mola, Ali alikuwa chini ya utii wako na utii wa Mtume wako, inua jua tena ili aweze kusala sala ya alasiri’.
Mwenyezi Mungu hapo hapo akaikubali dua ya mpenzi wake; Mtume, jua likachomoza tena (baada ya kuwa limekuchwa) na likatandaza mwangaza nyikani na milimani. Watu wakashuhudia muujiza huu wa Mtume (s.a.w.w) kwa macho yao. Kwa hiyo Ali akatawadha na kuswali.

Abu Jaafar al-Tahawi anaandika katika Mishkil-ul-Athaar, hadith inayotokana na Asma bint Umair amesema, alipowasiri Mtume kituo cha Sahba akaswali sala ya adhuhuri, tena akamtuma Ali kwa kazi ya dharura, aliporejea Ali, Mtume alikuwa amekwisha swali Alasiri. Mara Ali alipofika Mtume (s.a.w.w) akajilaza juu ya miguu ya Imam Ali (a.s) na akalala mpaka jua lilipokuchwa. Alipoamka na akaarifiwa kuwa Ali hakusali alasiri. Mtume (s.a.w.w) aliomba dua kwa Allah (s.w) akisema, “Mola wangu, Mtumwa wako Mahsusi Ali amejitolea nafsi yake kwa ajili ya Mtume wako, tafadhali rejesha jua lichomoze tena kwa ajili yake”.

Asma akaongeza kusema, ghafla jua likachomoza na mwangaza wake ukaangaza juu ya ardhi na milima, Ali (a.s) akatawadha na kuswali alasiri, kisha jua likazama tena.


Qadhi Ayadhi naye ameiandika hadith hii katika kitabu chake kiitwacho Kitabush-Shifa.

Comments