KUTHIBITISHA RISALA (UJUMBE) NA
WAHYI WA MTUME MUHAMMAD (S.A.W).
Mtume Muhammad (s.a.w) ni mtu
aliyekuwa hakusoma, na hakuonekana kukaa na watu Maulamaa, lakini jambo
lililowashangaza baadhi ya watu ni kwamba Mtume huyo alikuwa akiwatolea watu
simulizi na historia zinazohusiana na Mitume waliopita, kwa mfano, historia ya
Nabii Ibrahimu, Yussuf, Mussa, na Issa (a.s), mtu ambaye hakusoma wala hakuwa
na elimu yoyote ni muhali kujua habari muhimu (historia), kama hizo. Kwa hiyo
historia kama hizo zilizomo ndani ya Qur-an ni zenye kustaajabisha na
kuleta maajabu, na hiyo basi ni dalili kubwa ya kuthibitisha wahyi na ujumbe wa
Mtume Muhammad (s.a.w).
Qur-ani pia inathibitisha hayo
katika Surat Yussuf Aya ya 2-3, pale Allah (s.w) anaposema:- Hakika sisi
tumeiteremsha Qur-an kwa Kiarabu ili mpate kufahamu.
Sisi tunakusimulia simulizi nzuri
kwa kukufunulia Qur-an hii, na hakika ulikuwa kabla ya haya ni miongoni mwa
wasio na habari (hizi).
Aya hizo zinatilia mkazo na
kusisitiza kuwa (Mtume Muhammad (s.a.w) hakuwa na habari yoyote kuhusiana na
simulizi hizo, na Mwenyeezi Mungu alimjulisha na kumpa habari hizo kwa njia ya
Wahyi. Hii basi ndio dalili ya kuthibitisha kuwepo kwa Wahyi.
Kwa hiyo ujuzi na elimu yote
aliyokuwa nayo Mtume Muhammad (s.a.w.w) alivipata moja kwa moja toka kwa
Mwenyezi Mungu na hakuna Mtu anayeweza kusema kuwa Mtume alikuwa mwanafunzi
wake.
Comments
Post a Comment