MAONI YA MAWAHHABI NA MASALAFI KUHUSU UKHALIFA

MAONI YA MAWAHHABI NA MASALAFI KUHUSU UKHALIFA
Maoni yao juu ya Ukhalifa yanaeleweka, nayo ni kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.) alificha na hakumbainisha yeyote kushika Ukhalifa, lakini watu wenye hekima miongoni mwa Masahaba walikusanyika ndani ya Klabu ya bani Saidah na wakamtawalisha Abubakr ashike mahala pa Mtume (s.a.w.), na hiyo ni kwa sababu Mtume (s.a.w.) alimuachia kusalisha wakati wa maradhi yake, basi wakasema: Mtume wa Mwenyezi Mungu alimridhia Abubakar kwa ajili ya jambo la dini yetu basi ni kwa nini sisi tusimridhie kwa mambo ya dunia yetu?
Hivyo basi kauli ya Mawahhabina Masalafi kwa ufupi imefungamana na vifungu vifuatavyo:
1). Mtume (s.a.w.) hakumbainisha yeyote.
2).  Ukhalifa hauwezi  kusihi  isipokuwa kwa njia ya mashauriano.
3). Kumtawalisha Abubakr ni jambo lililotendeka kupitia Masahaba wakubwa.
Bila shaka haya ndiyo yalikuwa maoni yangu wakati nilipokuwa nikifuata Madhehebu ya Shafii, na nikiyatetea kwa nguvu zote nilizopewa na nikiyatolea dalili ya aya zinazohusu kushauriana, na nilikuwa nikijaribu kwa uwezo wangu kueleza kuwa dini ya Kiislamu ni dini yenye demokrasia katika maamuzi na kwamba yenyewe ndiyo iliyoanza kuweka msingi huu wa kibinaadamu, msingi ambao mataifa yaliyoendelea yanajivunia.
Zaidi ya hapo nilikuwa nikisema, "Ikiwa mataifa ya Magharibi hayakupata kuutambua utaratibu huu wa jamhuri mpaka katika karne ya kumi na tisa, basi bila shaka Uislamu umeyatangulia mataifa hayo na kuufahamu utaratibu huo tangu karne ya sita.
Lakini baada ya kukutana kwangu na wanachuoni wa Kishia na kusoma vitabu vyao na kuzichunguza hoja zao zenye kukinaisha, hoja ambazo zimo ndani ya vitabu vyetu nilibadili maoni yangu ya mwanzo pale nilipopambanukiwa na hoja zilizo wazi, kwani haiwezekani kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu kuuacha umma bila ya Imam (kiongozi) kwani yeye Mwenyezi Mungu ndiye asemaye: "Bila shaka wewe ni muonyaji, na kila kaumu inaye muongozaji".
Kama ambavyo haistahiki kabisa kwa mujibu wa huruma yake Mtume kuuacha umma wake bila mchungaji na hasa tutakapofahamu ya kwamba Mtume alikuwa akichelea utengano[23] wa umma wake na kurudi kinyume nyume[24] na kushindania dunia[25] kisa cha kuuana wao kwa wao[26] na kufuata nyendo za Mayahudi na Wakristo[27]
Na Iwapo Ummul-Muuminina Aisha binti Abubakr alimtumia ujumbe Umar bin Al-Khattab wakati alipopigwa dharuba ya upanga (iliyopelekea kifo chake) akamwambia:   
 "Mtawalishe mtu juu ya umma wa Muhammad (kabla hujafa) na usiwaache watu hivi hivi tu, hakika mimi nachelea fitina juu yao."
Taz: Al-Imamah wa Siyasah.
Na iwapo Abdallah bin Umar naye anaingia ndani kwa baba yake alipokuwa kapigwa dhoruba hiyo ya upanga na kumwambia: "Hakika watu wanadai kwamba wewe humtawalishi mtu (baada yako) basi waonaje lau ungekuwa na mchungaji wa ngamia au mchungaji wa mbuzi kisha akaja kwako na akaiacha mifugo hiyo bila shaka itapotea, basi usimamizi wa watu ni jambo muhimu zaidi."
Taz: Sahih Muslim Juz. 6 uk. 5, Baabul-Istikhlafi wa Tarkih.
Na kama Abubakr mwenyewe naye ndiye yule Waislamu walimtawalisha kwa mashauriano yeye ndiye anayebomoa msingi huo na haraka anamtawalisha Umar baada yake ili kwa tendo hilo akate mizizi ya utengano wa hitilafu na fitna. jambo hili la Abubakr kumtawalisha Umar baada yake, Imam Ali (a.s.) alilitambua mapema wakati ule Umar alipomlazimisha Imam Ali ampe Baia Abubakar, basi Imam Ali alisema kumwambia Umar:
"Niandae nafasi ili wewe uwe na hisa, na leo hii nimuimarishe ili kesho akurudishiye"!
Taz: Al-Imamah Was-Siyasah cha ibn Qutaibah Juz.l uk.18.
Basi mimi nasema, "Ikiwa Abubakr hayaamini mashauriano, ni vipi sisi tutaamini kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.) aliliacha jambo hili bila kumuweka mtu, na je tuseme Mtume alikuwa hakijui kile walichokuwa wakikijua kina Abubakr, bibi Aisha na Abdallah bin Umar? Na ni kitu ambacho watu wote wanakitambua moja kwa moja nacho ni kutokea hitilafu ya maoni na kila mmoja kutamani namna yake iwapo suala la kuamua lingeachwa mikononi mwao na hasa pale jambo lenyewe litakapohusu uongozi na kukalia madaraka ya Ukhalifa".
Rejea zingine:
[24]- Sahihi Bukhar Juz. 7 uk. 209 Babul-Haud na Juz. 5 uk. 192.
[25] Sahihi Bukhari Juz. 4 uk. 63.
[26]-Sahih Bukhar Juz. 7 uk. 112.

[27]-Sahih Bukhar Juz. 4 uk. 144 na Juz. 8 uk. 151

Comments