QUR’AN NA HADITH (SUNNAH) ZA
MTUME NDIO VYANZO PEKEE VYA SHERIA KWA MUISLAMU.
Qur’ani tukufu na Hadith, ndivyo
vitu viwili vya kimsingi ambavyo vinaunda Sheria za Kiislamu na kuzihakikisha,
na ni kutokana na vitu viwili hivyo ndipo misingi yote ya dini inaporejea.
Hata hivyo, ni Qur’ani tukufu tu
ndiyo marejeo makubwa ambayo Hadith zinategemea. Kwa ajili hiyo, Hadith
hazitofautiani au kupingana na Qur’ani ambayo inaaminiwa kuwa ndiyo asili ya
ukweli wote.
Miongoni mwa maudhui yenye maana
sana ya Qur’ani tukufu, ni kuwa inaeleza kanuni na Sheria zote za mwanzo
kusaidia watu ili waweze kupanga vizuri maisha yao, na hivyo kuweza kubadilisha
desturi zilizokuwa zikifuatwa. Kwa maana hiyo Qur’ani imehifadhi haki za kila
mmoja, na za jamii, imefanya kuenea kwa uadilifu, imewapa watu moyo wa kuishi
pamoja kwa ushirikiano na ihsani, na imeweka kipimo cha kumcha Mwenyezi Mungu
kuwa ndiyo tofauti pekee baina ya watu.
Hadith ni chochote kile ambacho
Mtume (s.a.w.w.) amekitenda na ambacho si Qur’ani; au mambo ambayo yamemfikia
kupitia kwa ufahamu wake au maono, na kuthibitishwa na Mwenyezi Mungu.
Kwa hiyo (Sunnah) inakusanya
vitendo na maneno yanayohusika na ufafanuzi wa itikadi, Swala au ibada
nyinginezo, pia kulingana na uhusiano mwema baina ya ndugu, kumfundisha
mwenendo mzuri, na kuamrisha mambo mema na kukataza maovu.
Kwa hivyo chochote kilichotendwa
na Mtume (s.a.w.) katika hali kama hiyo, huchukuliwa kama sunnah, na watu
wanatakiwa kukifuata. Chochote kile ambacho hakihusiani na hayo yaliyotajwa
hapo awali, kama vile kula, kunywa, au kuvaa nguo, hakichukuliwi kuwa ni
sunnah, na watu hawalazimiki kukifuata.
Mtume (s.a.w.w.) amesema:
“Hakika mimi ni mwanaadamu, pindi nitakapowaamrisha jambo linalohusiana na dini
yenu, lifuateni, na nitakapowaamrisha jambo kutokana na maoni yangu, basi
kumbukeni kuwa mimi ni mwanaadamu.”
Ushahidi wa jambo hili ni
ushauri ambao Mtume (s.a.w.) alizoea kuutoa kuhusiana na kutafuta tiba ya
baadhi ya maradhi. Ushauri ambao hakuletewa wahyi ila ni kutokana na uzoefu
alioupata kutokana na kuishi katika mazingira ya kibinaadamu.
Ametaja Abu Daud katika Isnadi
yake, kutoka kwa Usama kwamba: “Nilikwenda kwa Mtume (s.a.w.) naye alikuwa
ameketi na maswahaba zake, nao walikuwa (wametulia) kama kwamba kuna ndege juu
ya vichwa vyao, nikawatolea salaam, kisha nikaketi.
Wakaja mabedui kutoka huku na
huko wakasema: “Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, je tunaweza kujitibu?”
Mtume (s.a.w.) akasema: “Mnaweza
kujitibu, kwani Mwenyezi Mungu Mtukufu hakuumba ugonjwa pekee ila ameumba na
dawa yake, isipokuwa ugonjwa wa aina moja tu, kifo.”
Hadith nyingine iliyopokewa
kutoka kwa Umar Bin Dinar imetaja jambo hilo (pia).
Siku moja Mtume (s.a.w.)
alimtembelea mgonjwa, akawaambia nduguze, “Mwiteni daktari,” mmoja wao akasema,
“hata nawe pia wasema hivyo ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?!”
Mtume akasema: “Ndiyo, kwani
Mwenyezi Mungu Mtukufu hakuumba maradhi ila ameumba na dawa yake.” Kitendo cha
Mtume (s.a.w.) cha kuwataka ndugu za wagonjwa kumwita daktari kinaonyesha
kwamba utabibu wa madawa si miongoni mwa mambo aliyofunuliwa (wahyi) kutoka kwa
Mwenyezi Mungu, na ni kwa sababu hii ndipo akawashauri watu kufuata ushauri wa
daktari pale unapohitajika.
Pia hali hiyo inahusiana na
jinsi alivyokuwa akivaa na kula, ilivyokuwa ikilingana na tabia za wakati wake
na mahali alipoishi. Na lau kama angeishi katika mazingira na wakati tofauti,
basi pengine angestawisha desturi zingine.
Kwa hivyo basi, Sunnah (Hadith)
inafafanua Qur’ani, inachambua hukmu zake, inaikamilisha, inaelezea na kuamua
kuhusu mipaka ambayo inatawala kanuni zake kamili, na inafafanua sehemu zenye
kutatanisha.
Na endapo itaongezea chochote,
ziada hiyo haiwezi kupingana na misingi ya kanuni za Qur’ani. Kwa hivyo
uhusiano wa Sunnah na Qur’ani ulivyo ni kama hali ya kiongozi na mfuasi. Kwa
ajili hiyo, Hadith inafuata kile kilichokuja katika Qur’ani na inaambatana nacho
moja kwa moja.
Inadhihirika wazi sasa, kwa nini
Qur’ani inatangulia Sunnah, na kuchukuliwa kuwa ni msingi wa Uislamu, wakati
ambapo Sunnah inaikamilisha Qur’ani kwa kanuni.
Kwa hiyo tujifunze Sunnah sahihi
na tuzifuate, na matendo mengine yanayonasibishwa na Mtume lakini yanapingana
na Qur’an au hadhi ya Mtume basi tuachane nayo.
Comments
Post a Comment