QUR’AN NA HADITH (SUNNAH) ZA MTUME NDIO VYANZO PEKEE VYA SHERIA KWA MUISLAMU

QUR’AN NA HADITH (SUNNAH) ZA MTUME NDIO VYANZO PEKEE VYA SHERIA KWA MUISLAMU.
Qur’ani tukufu na Hadith, ndivyo vitu viwili vya kimsingi ambavyo vinaunda Sheria za Kiislamu na kuzihakikisha, na ni kutokana na vitu viwili hivyo ndipo misingi yote ya dini inaporejea.
Hata hivyo, ni Qur’ani tukufu tu ndiyo marejeo makubwa ambayo Hadith zinategemea. Kwa ajili hiyo, Hadith hazitofautiani au kupingana na Qur’ani ambayo inaaminiwa kuwa ndiyo asili ya ukweli wote.
Miongoni mwa maudhui yenye maana sana ya Qur’ani tukufu, ni kuwa inaeleza kanuni na Sheria zote za mwanzo kusaidia watu ili waweze kupanga vizuri maisha yao, na hivyo kuweza kubadilisha desturi zilizokuwa zikifuatwa. Kwa maana hiyo Qur’ani imehifadhi haki za kila mmoja, na za jamii, imefanya kuenea kwa uadilifu, imewapa watu moyo wa kuishi pamoja kwa ushirikiano na ihsani, na imeweka kipimo cha kumcha Mwenyezi Mungu kuwa ndiyo tofauti pekee baina ya watu.
Hadith ni chochote kile ambacho Mtume (s.a.w.w.) amekitenda na ambacho si Qur’ani; au mambo ambayo yamemfikia kupitia kwa ufahamu wake au maono, na kuthibitishwa na Mwenyezi Mungu.
Kwa hiyo (Sunnah) inakusanya vitendo na maneno yanayohusika na ufafanuzi wa itikadi, Swala au ibada nyinginezo, pia kulingana na uhusiano mwema baina ya ndugu, kumfundisha mwenendo mzuri, na kuamrisha mambo mema na kukataza maovu.

Kwa hivyo chochote kilichotendwa na Mtume (s.a.w.) katika hali kama hiyo, huchukuliwa kama sunnah, na watu wanatakiwa kukifuata. Chochote kile ambacho hakihusiani na hayo yaliyotajwa hapo awali, kama vile kula, kunywa, au kuvaa nguo, hakichukuliwi kuwa ni sunnah, na watu hawalazimiki kukifuata.

Mtume (s.a.w.w.) amesema: “Hakika mimi ni mwanaadamu, pindi nitakapowaamrisha jambo linalohusiana na dini yenu, lifuateni, na nitakapowaamrisha jambo kutokana na maoni yangu, basi kumbukeni kuwa mimi ni mwanaadamu.”
Ushahidi wa jambo hili ni ushauri ambao Mtume (s.a.w.) alizoea kuutoa kuhusiana na kutafuta tiba ya baadhi ya maradhi. Ushauri ambao hakuletewa wahyi ila ni kutokana na uzoefu alioupata kutokana na kuishi katika mazingira ya kibinaadamu.

Ametaja Abu Daud katika Isnadi yake, kutoka kwa Usama kwamba: “Nilikwenda kwa Mtume (s.a.w.) naye alikuwa ameketi na maswahaba zake, nao walikuwa (wametulia) kama kwamba kuna ndege juu ya vichwa vyao, nikawatolea salaam, kisha nikaketi.
Wakaja mabedui kutoka huku na huko wakasema: “Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, je tunaweza kujitibu?”
Mtume (s.a.w.) akasema: “Mnaweza kujitibu, kwani Mwenyezi Mungu Mtukufu hakuumba ugonjwa pekee ila ameumba na dawa yake, isipokuwa ugonjwa wa aina moja tu, kifo.”
Hadith nyingine iliyopokewa kutoka kwa Umar Bin Dinar imetaja jambo hilo (pia).

Siku moja Mtume (s.a.w.) alimtembelea mgonjwa, akawaambia nduguze, “Mwiteni daktari,” mmoja wao akasema, “hata nawe pia wasema hivyo ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu?!”
Mtume akasema: “Ndiyo, kwani Mwenyezi Mungu Mtukufu hakuumba maradhi ila ameumba na dawa yake.” Kitendo cha Mtume (s.a.w.) cha kuwataka ndugu za wagonjwa kumwita daktari kinaonyesha kwamba utabibu wa madawa si miongoni mwa mambo aliyofunuliwa (wahyi) kutoka kwa Mwenyezi Mungu, na ni kwa sababu hii ndipo akawashauri watu kufuata ushauri wa daktari pale unapohitajika.

Pia hali hiyo inahusiana na jinsi alivyokuwa akivaa na kula, ilivyokuwa ikilingana na tabia za wakati wake na mahali alipoishi. Na lau kama angeishi katika mazingira na wakati tofauti, basi pengine angestawisha desturi zingine.

Kwa hivyo basi, Sunnah (Hadith) inafafanua Qur’ani, inachambua hukmu zake, inaikamilisha, inaelezea na kuamua kuhusu mipaka ambayo inatawala kanuni zake kamili, na inafafanua sehemu zenye kutatanisha.

Na endapo itaongezea chochote, ziada hiyo haiwezi kupingana na misingi ya kanuni za Qur’ani. Kwa hivyo uhusiano wa Sunnah na Qur’ani ulivyo ni kama hali ya kiongozi na mfuasi. Kwa ajili hiyo, Hadith inafuata kile kilichokuja katika Qur’ani na inaambatana nacho
moja kwa moja.

Inadhihirika wazi sasa, kwa nini Qur’ani inatangulia Sunnah, na kuchukuliwa kuwa ni msingi wa Uislamu, wakati ambapo Sunnah inaikamilisha Qur’ani kwa kanuni.

Kwa hiyo tujifunze Sunnah sahihi na tuzifuate, na matendo mengine yanayonasibishwa na Mtume lakini yanapingana na Qur’an au hadhi ya Mtume basi tuachane nayo. 

Comments