FAIDA ZA DINI NI ZIPI?

FAIDA ZA DINI NI ZIPI?
Zipo sababu nyingi zimfanyazo mwanadamu ahitaji Dini.
1. Sote twajua kuwa mwanadamu ni mnyama ahitajiye kuishi kijamii pamoja na wenzake. Kila mtu anategemea mamilioni ya watu wenzake kwa maisha yake na kwa mahitaji muhimu ya hayo maisha yake. Pia tunajua kuwa kila jamii inahitaji  sheria fulani fulani ili kuzuia dhulma na kuhifadhi haki ya kila mtu katika jamii hiyo. Lakini basi swali lifuatalo ni hili, ni nani aliye na haki ya kutunga Sheria hizo? Mtu mmoja? (mtu huyo na awe mfalme au mtawala wa Kiimla)! Jibu ni “Hapana.” Yeye hataweza, maana kwa ajili ya silika za kibinadamu, atatunga sheria kwa kufuatana na tamaa yake ya kibinafsi.
Kikundi cha watu? (Watu hao na wawe wa kikundi cha Utawala wa watu wa koo Bora au wa kikundi cha  kidemokrasi)! Jibu ni kuwa, “Hawa pia hawataweza kuifanya  kazi hiyo ipasikavyo, maana kila mmoja wao hawezi  kujiepusha na uamuzi usio sawa na wingi wa uamuzi usio sawa, hauwezi kupatana na uamuzi ulio sawa.
2. Vile vile ni dhahiri kuwa hakuna kikundi cha watu kiwezacho kujiepusha na kujitia katika tamaa za kibinafsi. Kwa mfano katika siku za utawala wa kikoloni, mabunge na halmashauri  za Makoloni zilikuwa zikitunga sheria kufuatana na  mapendekezo ya watawala wa Kizungu. Siku hizi, mabunge na Halmashauri hizo hizo hutunga sheria kufuatana na  mapendekezo ya wananchi. Kujali ubinafsi kulikuwa na bado kungali jambo muhimu la kutunga sheria duniani pote.
3. Zaidi ya hapo hakuna mtu au kikundi cha watu chenye uwezo wa kutunga sheria za mambo mengi na ambazo zimo katika msingi wa usawa na uadilifu kamili.
Kwa sababu hiyo, ni lazima sheria hizo zitungwe na yule ambae ni mbora kuliko mwanadamu, ambae hana chochote cha kupoteza au cha kufaidika nacho kutokana na sheria hizo, na ambae kila mwanadamu ana uhusiano wa aina iliyo sawa kwake.
NI ALLAH pekee ndiye asiyependelea na ni mkamilifu. Kwa sababu hiyo  tunawajibikiwa kuwa na dini.
4. Zaidi ya hapo ni kuwa, sheria na desturi zilizotungwa na  mwanadamu zina upungufu mmoja mbaya sana: Sheria na desturi hizo haziwezi kuzuia matendo ya jinai. Upungufu huu, hukufanya kuwepo kwa sheria za aina hii kuwa kusiko na faida yoyote.
Kwa mfano, mwizi anaingia nyumba isio na watu, katika  kijiji cha ughaibuni, usiku wa manane kwa ajili ya kutaka  kuiba vitu vyenye thamani. Yeye aelewa wazi kuwa hakuna mtu aiwakilishaye Serikali, kwa maili nyingi sana kutoka  nyumba hiyo. Hivyo ataona kuwa na usalama kutokana  na kukamatwa. Je! Katika hali hii, iko sheira ya serikali  ambayo itamzuia mwizi huyu kutimiza jinai hii? Jibu ni kuwa  “HAKUNA”.
Kusema kweli hakuna serikali itakayomzuia mtu huyu kuiba, lakini Dini inaweza. Dini iliyo ya kweli, kama tulivyoieleza hapo juu, huwafundisha watu kuwa yupo Mwenyezi Mungu, ambaye ajua kila kitu na anayeona kila kitu. Yeye Mwenyewe ni Mwadilifu na Mwema na anatutaka nasi tuwe waadilifu na wema; kuwa tunahusikana na matendo yetu mbele yake na tutakuja mpa hesabu ya matendo yetu baada ya kufa kwetu. Kama mtu anaiamini dini hiyo basi, hivyo (Na kwa hivyo tu) anaweza kujiepusha na kutenda dhambi, jinai na  kuwadhulumu watu wengine popote awapo.
Sheria za serikali zaweza kuzuia mtu kutenda matendo  mabaya ya wazi wazi na hata hivyo, ni katika muda na mahali  ambapo mikono ya serikali hiyo yaweza kupafika. Lakini  kumwamini Mwenyezi Mungu na dini, hutawala si matendo ya mwanadamu ya kiwazi wazi tu bali hata yale yaiiyojificha  na yaliyo mawazo ya moyoni pia.
Utawala huu, hauna mipaka kwa kutegemea mahali maalum au muda fulani, kwa sababu Mwenyezi Mungu yupo kila  mahali na anaona kila kitu.

5. Ili kuzielewa vizuri faida zilizo wazi wazi, ambazo jamii  yazipata kutokana na imani ya kuwepo Mwenyezi Mungu na dini, hebu jaribu kufikiria machafuko na ghasia ambazo  wanaadamu wangeliweza kujitia, kama imani ya kuwepo Mungu ingalitupiliwa mbali. Hakutakuwa na jamii yoyote.  Badala yake, kutakuwa na umati wa watu tu. Katika hali hiyo, kila mmoja anao uhuru wa kufanya chochote kile  akipendacho. Mtu atafikia kuwa hakuna Mungu, na hakuna maisha ya Akhera, na kuwa yeye amekuwepo hapa duniani  kwa bahati ya hali ya asili iliyojitokeza tu. Na pia anajua  kuwa muda wa maisha ni mfupi. Kwa hivyo, kikawaida  atashawishika na kuyafaidi maisha kwa kadri iwezekanavyo bila ya kujali kitu chochote kile. Kitu atakacho kiwazia ni  kujaribu kuepuka kukamatwa akiwa anatenda jambo lolote baya, au kuonwa na serikali tu. Na wakati wowote  atakaojiona kuwa yu salama, hataacha kutenda jinai lolote ili kujikidhia tamaa zake, bila ya kujali dhara la tamaa yake hiyo kwa wenzake.

Comments