MTU WA KWANZA KUSILIMU

MTU WA KWANZA KUSILIMU
Ameeleza Ibn Hajar al-Asqalani katika kitabu chake al-Isabah, kwa namna ya maelezo ya wanavyuoni wengi, kuwa mtu wa kwanza  aliyeleta imani na kukubali dini ya Kiislamu ni Bwana Abul Hasan Ali bin Abi Talib. Ali alizaliwa miaka kumi (10) kabla ya “Bi’that” (kabla Mtume (s.a.w.w.) kutangaza Utume wake). Alilelewa katika mikono ya Mtume (s.a.w.w.) na hawakuachana (hawakufarakiana) maisha yao yote.

Abdul Malik Ibn Hisham katika kitabu chake alichoandika juu ya maisha ya Mtume, kinachoitwa Sirat Ibne Hisham, amehadithia hivi kwamba Ali ni mtu wa kwanza aliyemwamini Mtume (s.a.w.w.) na akaukubali Uislamu na yale aliyoteremshiwa Mtume: Umri wa Ali  alipoikubali dini ya Kiislamu ulikuwa miaka kumi (10). Katika neema aliyombariki Mwenyezi Mungu Ali ni kulelewa na Mtume chini ya uongozi wake wa haqqi kabla ya kudhihirika Uislamu. Baada ya Ali, Zaid Bin Harth akakubali Uislamu na akasali na baada ya huyu Zaid, Abu Bakr akaingia katika Uislamu.

Katika kitabu cha maisha ya Mtume Muhammad (s.a.w.w.) kiitwacho  Isteeab alichoandika Ibn Abdul Bir al-Maliki, amesema kwamba  Muhammad ibn Kaab Qarzi aliulizwa na watu, nani aliyeifuata dini ya Kiislamu kwanza, Ali au Abu Bakr. Akajibu: “Subhaanallah! Ali ndiye wa kwanza kukubali Uislamu”.
Baadaye Ibn Abdul Bir anaeleza: “Sisi hatuna shaka kwamba Ali ndiye wa kwanza miongoni mwa hawa wawili (Ali na Abu Bakr) kukubali Uislamu.

Zaidi ya haya Salman  al-Farsi, Abu Dhar, Miqdad, Khabbab, Abu Saeed Khudri na Zaid Bin Arqam wanashuhudia kwamba hakika Ali ni wa kwanza kukubali Uislamu na masahaba hawa wamemfadhilisha Ali juu ya masahaba wengineo.”

Comments