NI NANI BIN ABDUL WAHHAB

NI NANI BIN ABDUL WAHHAB
Yeye ni Muhammad bin Abdul Wahhab bin Sulayman bin Ally bin Muhammad bin Ahmed bin Rashid wa kabila la Banu Tamim. Alizaliwa mnamo mwaka 1115 A.H. (1703 A.D) katika mji wa Uyayna, katika nchi ya Najd iliyoko mashariki ya nchi ya Hijaz (nchi yenye miji ya Maka na Madina).
Kuna hadithi nyingi  za Mtume (s.a.w.) zinazowazindua Waislamu juu ya fitna na balaa la utovu litakalotokea katika dini kwa kuletwa na watu kutoka Najd. Wanachuoni  wengi wamehakikisha kuwa hadithi hizo zilikuwa zikimtabiri Muhammad bin Abdul Wahhab, na wazushi wengine waliotokea mapema kama vile Musaylimah al-Kadhdhaab, ambaye ni babu wamababu wa Mfalme Muhammad bin Saud aliyeasisi Saudi Arabia kwa  kushirikiana na Muhammad bin Abdul Wahhab na kwa msaada mkubwa wa Serikali ya Uingereza.
Katika  hadithi mojawapo ambayo Mtukufu Mtume (s.a.w.)  anamtabiri Muhammad bin Abdul Wahhab alisema: “Atakuja tokea Shetani kutoka (mji wa) Najd, atatia  msukosuko (mtikisiko) katika kisiwa (eneo) cha Arabuni kutokana na fitna yake”. (al-Fajr S’adiq uk.21)
Katika hadithi nyingine Mtume (s.a.w.) amesema: “Itatokea fitna kutoka huko”; huku akiashiria kwa  mkono wake mtukufu upande wa mashariki (yaani Najd).
Nchi ya Najd ndiyo ambayo Muhammad bin Abdul Wahhab alizaliwa. Na ndio nchi hiyo hiyo ambayo Mtume wa Mwenyezi Mungu alikataa kuiombea dua wakati alipofikiwa na wageni kutoka katika mji huo. Na hadithi inayozunguzia habari hiyo si tu kwamba  ni mashuhuri bali imenakiliwa pia na Wahhabi  wenyewe katika kitabu chao juu ya maisha ya Sheikh wao Muhammad bin Abdul Wahhab ambacho  kilichapishwa kwa idhini ya Mfalme Faisal. Jina la kitabu hicho ni “Sheikh Muhammad bin Abdul  Wahhab”. Katika kitabu hicho uk. 86 imenakiliwa  hadithi hiyo ambayo Mtume katika dua yake aliweka wazi ubaya wa watu watakaotoka Najd juu ya Uislamu.
Mtume (s.a.w.) alikuwa akiomba akisema:
 “‘Ewe Mola wangu! Tubarikie sisi katika Shamu na Yemen’. Wakasema (Watu wa Najd): ‘iombee na Najd yetu Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu’. (Mtume)  akakariri dua hiyo mara tatu akiiombea Shamu na Yemen na hali wao (watu wa Najd) wakisema iombee na Najd yetu Ee Mjumbe wa Mwenyezi Mungu. Mara ya nne (akajibu) akasema: ‘Huko (Najd siombei) ni mahala pa misukosuko na fitna’”.
Hadithi zote hizo zinaelezea jambo moja tu, nalo ni kutokea fitna kutoka Najd. Kwa kutaka kutimiza  ukweli wa maneno ya Mtume wake (s.a.w.), Mwenyezi  Mungu akauhakikisha usemi huu wa Mtume (s.a.w.). Akatokea Muhammad bin Abdul Wahhab,  akaungana na Muhammad bin Saud kwa tamaa ya mali na utukufu wa ufalme, na kutoridhika na milki yake ya Najd, wakazivamia ardhi za Hijaz;  wakamwaga damu kwa kiasi cha kutisha kwa ukatili  mkubwa kabisa na bila kujali watoto wadogo, vikongwe,  wanawake na watu kadhaa wasio kuwa na hatia yoyote.  Matendo yao mabaya ni pamoja na kupora mali za watu, ikiwa ni pamoja na kuwakufurisha Waislamu  waaminio na kuwalinganisha na wapagani wa Makka  waliokuwa wakiabudu masanamu; hali ya kuwa  Waislamu wale walikuwa wakimpwekesha Mwenyezi  Mungu.

Kwa kifupi, katika vitabu vya historia  Muhammad bin Abdul Wahhab amejulikana kama “Shaikh an-Najd”. Jina hili linakamilisha utabiri wa Mtume (s.a.w.) juu ya kutokea Sheitani kutoka Najd.

Kwani wanavyuoni wa Fiqhi (wanasheria wa Kiislamu) wanaposema “Shaikh an-Najd” huwa wanamkusudia Iblisi na ukisoma hadithi ile ya mwanzo utaona Mtume (s.a.w.) anasema “Atatokea Shetani kutoka Najd”. Basi hapana shaka kuwa aliyetajwa hapa ni Muhammad bin Abdul Wahhab. Basi namna gani Waislamu wanaweza kumfanya mtu aliyetajwa na kuitwa Shetani na Mtume wa Mwenyezi Mungu kuwa Imam wao? 

Comments