MADHARA YA KUTOIELEWA
DINI
Mara kwa
mara tunasikia maneno mabaya yakisemwa wazi wazi, ili kuipinga “Dini”. Maneno
haya yanatumiwa sana siku hizi, na Makomyunist. Maneno hayo ni:
i. Dini inapinga sayansi
ii. Dini ni
dawa iliyogunduliwa na mabeparili kuwatuliza watu wa tabaka linalodhulumiwa, na
kuwafanya watosheke na hali yao hiyo ya kimaskini; kwa usemi mwingine dini
ilikuwa kasumba ya kuwalazia watu.
iii. Dini hupunguza
maendeleo ya kimwili na kiakili.
Basi hebu
ngoja tuzichunguze hoja hizi. Habari hizi hizi
zimesemwa na Wazungu wengi (toka Karl Marx hadi Bertrand Russel) ambao
walikuwa na ujuzi wa dini moja tu, nayo ni Ukristo; hakika wametenda dhambi
kubwa ya kiakili, kwa kuona dini fulani, na kudhania kuwa dini zote (hata
Uislamu) ni lazima ziwe na fikara hizo hizo.
Hakika kwa
vyovyote vile maneno yao hayo kama si fikara
zilizotolewa kwa shabaha maalum, ni udanganyifu mtupu.
Ili kuueleza
kinaga naga usemi huo hapo juu, inatulazimu kuieleza kwa muhtasari tu hali ya
fikara za kikristo ilivyokuwa kuhusu ujuzi na maendeleo.
“Tangu karne
ya kumi na sita ya baada ya Nabii Isa (a.s.),
ulitokea ugomvi kati ya Kanisa na sayansi. Ugomvi huu mbaya sana
haukuanzwa na wanasayansi, ila ulianzwa na viongozi wa kikrsto; ambao walihofu kuwa dini yao ilikuwa
katika hatari kubwa ya kupoteza nguvu
zake miongoni mwa wakristo. Ngome ya mafundisho yao ilikuwa katika hatari ya
kuanguka.
Madhehebu
zote mbili (Wakatoliki na Maprotestanti) ingawa
zilikuwa zikigombana zenyewe kwa zenyewe, zilikuwa na msimamo mmoja kuhusu mapambano baina ya
mafundisho yao na njia za kimapinduzi za kisayansi, za Bwana Cupernicus, na
mwenzie bwana Galileo. Walifanya kile kile ambacho kila mdhalimu anayeogopa unyoge wake wa kiasili
angeliweza kukitenda. Mateso makali sana
yalitolewa kwa wanasayansi washupavu waliolipinga Kanisa na ambao walisema kuwa
kile wakijuacho kilikuwa ukweli mtupu.
“Kwanza
hatuna budi tumchukue Bwana Cupernicus (Nicolaus Koppernigk) aliyeishi kati ya
mwaka 1473-1545, maana yeye alikuwa
ndiye aliyeanzisha jambo hilo. Bwana huyu kwa muda mrefu hakuthubutu hata
kuchapisha kitabu chake kijulikanacho
kwa jina la On the Revolution of Heavenly Bodies (katika mzunguko wa sayari za Angani) kwa ajili ya
kuliogopa Kanisa. Mwishoni alifaulu kulituliza Kanisa kwa kukiandika kitabu
hicho kwa heshima ya Papa (afisa wa cheo
cha juu sana wa Kanisa Katoliki).
Mchapishaji
wa kitabu hiki aliandika utangulizi kuthibitisha kuwa maelezo juu ya mzunguko
wa dunia ni jambo linalokubaliwa tu,
wala si jambo lililothibitishwa kabisa. Kwa
maneno ya Bwana Bertrand Russel, ‘Kwa muda fulani, mbinu hizi zilitosha,
na ni kutokana na wito wa kijasiri wa Bwana Galileo (wa kuwaita wana dini kuja
kushindana na Wanasayansi) ambao ulileta
shutma za wakati uliopita wa Bwana Cupernicus’.” (rejea katika kitabu kiitwacho
Religion and Science).
“Bwana
Luther pia, aliupinga ‘utaratibu’ wa Bwana Cupernicus kwa kutumia njia za
Kitheolojia (za kiujuzi wa Sifa na Tabia za Mwenyezi Mungu).
“Mwanasayansi
mwingine, Bwana Galileo Galilei aliyeishi kati ya mwaka 1564-1642 Masihiyya,
ingawa alikuwa rafiki wa Papa Urban
VIII, alitiwa katika jela ya Mahakama ya kuhukumu kesi za wazushi wa mambo ya
kidini, kwa amri ya Papa huyo huyo na kutishiwa atapata mateso makali kama
hataacha mafundisho yake hayo. Makosa ya Galileo yalikuwa kuunga mkono
mafundisho ya Copernicus kutokana na uchunguzi alioufanya kwa darubini yake.
Kwa upande wa Kanisa, uchunguzi huu ulikuwa mgumu zaidi kupambana nao, kuliko ile elimu ya
kimaandishi tu ya Bwana Copernicus.
“Mwana
Sayansi mwingine Bwana Giardino Bruno aliyeishi kati ya mwaka 1549-1600
Masihiyya, alikuwa madhabuha mwingine wa ukatili uliotendewa wanasayansi. Bwana
huyu alichomwa hali ya kuwa yu hai.
“Bwana
Bertrand Russel, ameandika katika kitabu chake
kiitwacho Religion and Science hivi: ‘Wataalamu wa Elimu Lahuuti hawakuchelewa kusema kuwa, mafundisho
hayo mapya yatafanya yale mafundisho ya kuchukua umbo la kiutu (incarnation, kwa mfano Yesu kuwa ni Mungu
aliyegeuka katika umbo la Binaadamu) kuwa ni vigumu kuaminika’.” (rejea katika
kitabu kiitwacho Religion and Science).
“Hivyo
mahakama ya hukumu za wazushi wa Kidini, ilitangaza haya yafuatayo kuwa ndiyo
ukweli. “Usemi wa kwanza, kuwa jua ndio kitovu (centre) cha Ulimwengu na kuwa
jua haliizunguki dunia ni wa kijinga,
kipuuzi, usio kweli hata kidogo katika Elimu lahuuti na ambao ni uzushi mtupu,
maana hauafikiani na maandishi
Matakatifu..... Usemi wa pili usemao kuwa dunia si kitovu cha ulimwengu na kwa hiyo dunia ina
lizunguka jua ni upuuzi, ni uwongo
katika elimu ya hekima (filosofia) na kwa upande wa elimu Lahuuti, kwa ujumla
haitofautiani na imani sahihi.” (rejea
katika kitabu kiitwacho Religion and Science).
“Na kwa
kuongezea zaidi, Kasisi wa shirika la Jesuit aliyeitwa Melchior Inchofer
ilimbidi aongezee kusema wazo lihusulo
mzunguko wa dunia ni uzushi mtupu, lichukizalo zaidi, lenye madhara
zaidi na lenye kuaibisha zaidi. Kutulia kwa dunia ni kutakatifu mara tatu; hivyo basi hoja
zipingazo maisha ya milele ya roho, kuwepo kwa Mwenyezi Mungu na wa Mungu
kuchukua umbo la kiutu ni lazima
zikubaliwe upesi kuliko hoja
zithibitishazo kuwa dunia inasogea. (rejea katika kitabu kiitwacho
Religion and Science).
Kwa sababu
ya kukabiliwa na dhuluma kali, Wanasayansi
waliueleza Ukristo, kuwa ni “imani isiyo pendelea mambo ya kiakili na isiyopendelea mambo ya Kisayansi;
ni ushirikina na ni kitu kirudishacho nyuma maendeleo ya binaadamu.”
Jambo la
kustaajabisha ni kuwa wameichukulia kila dini kwa ujumla kuwa ni sawa na
Ukristo. Kwa hakika Uislamu hauwezi kuwekwa
miongoni mwa dini ‘zisizoafikiana na sayansi, zisizo za kihoja, au zisizoafikiana na maendeleo ya
kibinaadamu.’
Ukweli ni
kuwa Uislamu unaafikiana na sayansi katika mambo mengi kuliko ukristo na pia
Uislamu unawahimiza waumini wake wafikiri kila hoja ijayo mbele yao na
wasikubali kukubali hoja kibubusa.
Comments
Post a Comment