Je! ni Muislamu gani anayepinga au
kutokuwa na haja ya kuwa pamoja na hao wakweli?
Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
(Antadhilla ihdaahuma fatudhakkira Ihdaahumal-Ukhra), "Mmoja wao akisahau
mwingine amkumbushe". (Qur'an 2:282).
Hivyo ninalazimika kukukumbusheni kwa
sababu ninahisi kuwa wengi wa wanadamu wamesahau na kutapatapa katika imani
zenye makosa au mapungufu.
Hawa wakweli ni akina nani?
Mtume Muhammad (s.a.w.w) anasema, "Nimeacha
miongoni mwenu vizito viwili, kitabu cha Mwenyezi Mungu na kizazi changu watu
wa nyumba yangu, vitu ambavyo mkishikamana navyo hamutapotea kamwe baada
yangu".
Basi hadithi iko wazi mno katika
kuonyesha upotovu wa yeyote asiyeshikamana na viwili hivyo kwa pamoja (yaani
kitabu cha Mwenyezi Mungu na kizazi cha Mtume). Hawa Ahlulbayt wa Mtume ndio
watu wakweli kuliko wote duniani, na tunaposhindwa kujua tafsiri ya Qur’an au
jambo lolote la Sunnah au mengineyo ni lazima turejee kwa watu hawa watukufu na
sio kwa watu wengine.
Endapo kama mtu anataka kuongoka kwa
fadhila za Mwenyezi Mungu Mtukufu, ni lazima ashikamane na kitabu cha Mwenyezi
Mungu na kizazi cha Mtume (s.a.w.).
Basi namshukuru Mwenyezi Mungu ambaye
ametuongoa kwenye ukweli huu na kuwa tusingeongoka lau Mwenyezi Mungu
asingetuongoa. Bila shaka wamekwisha kutufikia Mitume wa Mola wetu wakiwa na
ukweli (tunaowajibika kuufuata).
Comments
Post a Comment