MZEE ABU TALIB BIN ABDUL MUTALIB (a.s)

MZEE ABU TALIB BIN ABDUL MUTALIB (a.s)

Bwana Abu Talib (a.s.) ni baba mzazi wa Amir al-Muminiin Imam Ali ibn Abi Talib (a.s.). na yeye ndio mlezi wa Mtume Muhammad (s.a.w.w).

Bwana Abu Talib (a.s.) wakati wake mwingi  ameutumikia Uislamu na vile vile katika kumhifadhi na  kumnusuru Mtume (s.a.w.w.). Katika hali hii yeye ameweza  kuvumilia hasira na ukali wa chuki za kabila lake la Maquraish kiasi cha yeye na hao wachache walipokuwa wametolewa nje ya mji wakakaa katika Sha’b-i-Abu Talib na wakastahimili matatizo na dhiki zote na wakaweza kufanya subira ya hali ya juu (wakati huo Abubakar alikuwa mjini akila kuku kwa mrija na Umar alikuwa hajasilimu).

Kwa  hakika ni kwamba wakati huo ndio uliokuwa wa harakati na  mikakati mipya ya mapinduzi ya Kiislam ambayo yalikuwa  yakitekelezwa na Mtume (s.a.w.w.).

Sha’b-i-Abu  Talib kisa chake hicho kinaonyesha wazi uhalifu uliokuwa  ukifanywa na Maquraish kisiasa, kiuchumi na kimaisha na 
kijamii vile vile dhidi ya Mtume (s.a.w.w.) na watu wake.

Katika hali ngumu kabisa kama hizi na zinginezo tulizonazo katika  historia Bwana Abu Talib kwa nyakati mbalimbali ameweza  kujitolea yeye mwenyewe kumnusuru na kumlinda Mtume (s.a.w.w.) na vile vile amewaamrisha wanawe Ali (a.s.) na Jaafar (a.s.) wawe daima wakijitolea kwa ajili ya kumnusuru na  kumwokoa Mtume (s.a.w.w).

Kwa muhtasari kabisa tunaona kuwa maisha yake yote alikuwa ameshajitolea katika kuunusuru na kueneza Uislamu na kumwokoa na kumkinga Mtume (s.a.w.w.) kwa sababu tu yeye alikuwa amekwisha ongoka na kupata  hidaya ya Islam. Yeye wakati wa mwisho wa pumzi yake alikuwa  akiwasisitiza na kuwahimiza watoto na jamaa zake wawe daima mbele katika kumnusuru na kumkinga na kumuunga mkono  Mtume Muhammad (s.a.w.w.) katika kueneza Uislamu.
Na vile vile kwa kifo chake (ambacho kilikuwa baada ya kifo cha  Bi. Khadijat-il-Kubra) Mtume (s.a.w.w.) alikuwa amehuzunika mno kiasi kwamba alikuwa ameutangaza mwaka huo kuwa ni aamul huzuni yaani mwaka wa huzuni kubwa.

Kwa kupata mwangaza huo bado tunaona katika vitabu vingine vya kihistoria vya madhehebu mengine yakiwa yanamtaja Bwana  Abu Talib kuwa ni mushrik na kuthubutu kumsema kuwa ni  kafiri. Kwa hakika tuhuma kama hizi katika historia ni njama  kubwa sana zilizofanywa na wamejaribu hao waliotoa tuhuma  hizo, kuthibitisha tuhuma zao kwa kupotosha aya za Qurani tukufu na  hadithi za Mtume (s.a.w.w.).

Madhumuni makubwa  ya hawa watoao tuhuma kwa kusema Bwana Abu Talib kuwa ni  mushrik na kafiri huku wakimchukulia yeye kuwa ni mtu mmoja wa kawaida na siri ya malengo yao ni kule kuthibitisha kuwa baba yake Imam Ali ibn Abi Talib (a.s.) alikuwa ni mushriki na kafiri ili waweze kumvunja nguvu Imam Ali (a.s.). Ni dhahiri kuwa ni jambo ambalo tunalielewa kuwa iwapo baba atapata pigo basi shida hiyo kubwa itamfikia na kumwathiri mtoto wake katika maisha na nyadhifa zake.

Lakini kama tulivyokwisha kuona kuwa malengo yao sio Bwana Abu Talib mwenyewe bali wao wanataka  kumdhoofisha na kumvunja nguvu Imam Ali (a.s) kuwa baba yake alikuwa hana imani na alikuwa mushriki na kafiri ili kwamba Imam Ali (a.s.) hali na maisha yake yawe na dosari kubwa.
Vyote tulivyokwisha kuvisoma hapo juu, usahihi wake au uwazi  wake unakuwa pale wakati tunapoona kuwa historia hii hii na waandishi hawa hawa na wanonakili riwaya hawa hawa ambao  wanatoa uamuzi kama huo kuhusu Abu Talib (a.s.) — wanakaa kimya kuhusu wazazi wao waliokuwa wakija daima mbele ya Imam Ali (a.s.) katika maisha yao — wao daima wamekuwa  wakiyeyuka mbele ya nuru ya Imam Ali (a.s.) kwa kutoweza  kustahimili nuru hiyo.


Tunaona kuwa waandishi hawa hawa na wanaoripoti riwaya hizi ndio wanaoandika fadhila zake lakini  tunashangaa kuona pamoja na kuandika sifa na fadhila na daraja  zake makabila yao na watu wao wanashindwa kupambanua  upotofu huu ulivyo ndipo hapo tunalazimika kufanya utafiti na kuchambua historia kwa undani kabisa pamoja na matukio na  riwaya na insha – Allah itatudhihirikia kuwa Abu Talib kamwe hakuwa mushrik wala kafiri.

Comments