IMAM ALLY (a.s) KATIKA VITA VYA BADRI

IMAM ALLY (a.s) KATIKA VITA VYA BADRI
Ilikuwa tarehe 17 ya mwezi wa Ramadhan mwaka wa pili Hijria ndipo kulitokea vita vya Badri kati ya waislamu na Maquraishi.

Vita hivyo vilitokana na waislamu kushambuliwa na makafiri hawa kwa sababu waislamu walikandamizwa sana walipokuwa Makkah na walikuwa wavumilivu. Waislamu walipohamia Madina na kupata waumini wengi kuliko kipindi walipokuwa Makkah. Makafiri walichukia sana na kutaka kuwafyeka waislamu na kuumaliza Uislamu.

Hivyo makafiri walifunga safari kuwafuata waislamu kwa ajili ya vita, kwa bahati nzuri waislamu kwa mara ya kwanza walipewa ruhusa na Allah wajitetee. Ndipo waislamu walipochukua silaha zao na kwenda pembeni ya mji wa Madina ambayo iliwapo njia ya kutokea Makkah ili wakabiliane na maadui hao huko pembeni ya Mji na hivyo kuzuia athari za vita visiwakumbe akina mama, wazee, walemavu na watoto.
Kwa ushahidi wa hili angalia ramani, utaiona Badri ipo karibu zaidi na Madina kuliko Makkah. Huo ni ushahidi kuwa waislamu walishambuliwa kwanza na ndipo walipolazimika kujitetea.

Katika vita hii waislamu walikuwa na jeshi dogo la askari 313 na Maquraishi walikuwa na jeshi kubwa lenye askari zaidi ya 950, yaani zaidi ya mara tatu ya waislamu.

Licha ya uchache wao waislamu walipata ushindi mkubwa kwa kuwauwa Maqraishi 70 na kuwateka wengine 70. Hata hivyo waislamu 22 nao waliuawa.

Hivi ndivyo Mwenyezi Mungu alivyowaahidi waumini kuwa ushindi uko upande wao licha ya udogo wao kiidadi. Ndipo Allah anasema katika Qur’an takatifu,  “Makundi mangapi madogo yameyashinda makundi makubwa kwa idhini ya Mwenyezi Mungu? Na Mwenyezi Mungu yuko pamoja na wenye kusubiri”(2:249).

Allah analizungumzia tukio la Badri kuwa, “(kumbukeni) mlipokuwa mkiomba msaada kwa Mola wenu, naye akakujibuni: kwa hakika mimi nitakusaidieni kwa Malaika elfu moja watakao fuatana mfululizo” (8:9).

Katika vita hii Mtume alikuwa amiri jeshi mkuu, Hamza bin Abdul Mutalib alikuwa kamanda mkuu na Imam Ally alikuwa ndiye komandoo wa kutegemewa zaidi kwa sababu Imam Ally peke yake aliwaua zaidi ya Maquraishi 35 tena akichagua makomandoo wao tu na kuwaacha madhaifu wao. Ndio maana utashangaa kwa nini vita vilimalizika mapema kwa kuuawa Maqraishi 70 tu?

Vilimalizika mapema kwa sababu kuu mbili:
1.  Mungu alikuwa ameshusha Malaika kuwaisaidia waislamu hivyo Maquraishi waliona waislamu kuwa ni wengi zaidi yao kwa maelfu.
2.  Makamanda na wataalamu wa vita waliotegemewa ndio waliokuwa wakiuawa zaidi, hivyo waliamini kuwa wasipokimbia watauawa wote.
Funzo.
Kama waislamu chini ya Mtume, walipokuwa vitani walichagua askari madhubuti na kuwaua, kisha huwaacha askari goigoi na kusababisha ushindi kupatikana bila kuua watu wengi. Je ....
a.  Mawahhabi wanaporipua watu wote bila kuchagua wamejifunza wapi mbinu hii ya vita?
b.  Kwa mfumo wa uripuaji kila eneo, ushindi utapatikanaje?
c.   Endapo kama unawaua watu wote, utamtawala nani?
d.  Kitu gani kinawafanya mawahhabi na masalafi wasiifute sunnah ya Mtume katika vita?

e.  Vita vya Mawahhabi na Masalafi kuawa kila mtu, hata waislamu ni Jihad kweli au sio?

Comments