MASUNNI WA MALIKI WANYOOSHA MIKONO KATIKA SWALA SAWA NA MASHIA

MASUNNI WA MALIKI WANYOOSHA MIKONO KATIKA SWALA SAWA NA MASHIA

Wafuasi wa Malik wanasema: “Ni Sunna kuachia mikono ndani ya Sala ya faradhi.”

Na kuna kundi kubwa la wanazuoni lililosema hivyo kabla yao, kati yao ni Abdullah bin Zubeiri, Saidi bin Al- Musayyabu, Saidi bin Jubairi, Atau, Ibnu Jariji, An-Nakhaiy, Hasani Al-Basriy, Ibnu Sirini na kundi la wanafiqihi. Na ndio msimamo wa Alay-thu bin Saad, isipokuwa yeye kasema: “Isipokuwa atakaporefusha kisimamo na akawa amechoka basi itambidi kufunga mikono.”

Na kauli iliyonukuliwa toka kwa Imam Al-Awzaiy ni hiyari kati ya kufunga mikono au kuachia.1

Mufti wa madhehebu ya Malik huko Ad-Dayaru Al-Hijaziya, Muhammad Abdu ameona kuwa kuachia mikono na kufunga ni Sunna toka kwa Mtume na kuwa muumini anaporefusha kisimamo ilihali kaachia mikono na akachoka basi anafunga mikono. Akasema kuwa kuachia mikono ni asili na kufunga ni tawi. 2

Ama Shia Imamiyah mashuhuri kwao ni kuwa ni haramu na hubatilisha Sala, na ni wachache sana wamesema ni makuruhu, kama vile Al-Halbiy ndani ya Al-Kafiy 3
Uchambuzi wa rejea:
1. Hadithi ya Sahl bin Saad. Kaipokea Bukhari.
2. Hadithi ya Wailu bin Hajar kaipokea Muslim na kainukuu Al- Bayhaqiy kwa njia tatu.
3. Hadithi ya Abdallah bin Mas’ud kaipokea Al-Bayhaqiy ndani ya Sunan yake na vitabu vingine.

Ufuatao ni uchambuzi wa Hadithi ya Sahl bin Saad.
Bukhari amepokea toka kwa Abu Hazimu toka kwa Sahl bin Saad amesema: Watu walikuwa wakiamrisha mtu aweke mkono wa kulia juu ya dhiraa yake ya kushoto ndani ya Sala. Abu Hazimu akasema: Silijui jambo hili, labda kama hilo litanasibishwa na Mtume.

Riwaya imebeba jukumu la kubainisha namna ya kufunga mikono, isipokuwa baada ya njia yake ya upokezi kukubalika tatizo linabakia kwenye hoja yake.

Wala riwaya haionyeshi Sunna ya kufunga mikono. Hilo ni kwa vigezo viwili:

Kwanza: Laiti kama Mtukufu Mtume angekuwa ndio muamrishaji wa kufunga mikono basi ni nini maana ya kauli “Watu walikuwa wakiamrisha” Hivi haikuwa ni sahihi kusema Mtume alikuwa akiamrisha? Hivi huoni kuwa hii ni dalili kuwa hukumu ya kufunga mikono ilianza baada ya kufariki Mtukufu Mtume kiasi kwamba makhalifa na magavana wao walikuwa wakiwaamrisha watu kufunga mikono kwa kudhania kuwa hali hiyo ndio iliyo karibu sana na unyenyekevu?

Na kwa ajili hiyo baada ya riwaya hiyo Bukhari akaweka mlango maalum kwa jina la mlango wa unyenyekevu.

Ibnu Hajar amesema: “Hekima ya muundo huu (kufunga mikono) ni kuwa ni sifa ya muombaji dhalili, nalo ni jambo linalomzuwia mtu kuchezacheza na liko karibu sana na unyenyekevu, Bukhari alizingatia hekima hii hivyo baada yake akaleta mlango wa unyenyekevu.

Kwa ibara nyingine ni kuwa: Kuamrisha kufunga mikono ni dalili ya kuwa watu katika zama za Mtume na muda mfupi baada ya zama zake walikuwa wanaswali kwa kuachia mikono, kisha baadaye ikazushwa fikra hii na hivyo wakawaamrisha watu kufunga mikono.

Pili: Hakika mwishoni mwa njia ya upokezi kuna kitu kinachounga mkono kuwa kufunga mikono ilikuwa ni kitendo cha waamrishaji wala si kitendo cha mwenyewe Mtukufu Mtume, kwani amesema:
Ismaili amesema: “Silijui jambo hili, labda kama hilo litanasibishwa kwa Mtume.” Hiyo ni kama tutasoma kwa tamko la kutomtaja mtendaji. Maana yake itakuwa yeye hajuwi kuwa jambo hilo ni Sunna ndani ya Sala isipokuwa linanasibishwa tu na Mtume, hivyo riwaya aliyoipokea Sahl bin Saad itakuwa imevushwa (Yaani mlolongo mzima wa wapokezi hadi kumfikia yeye haujatajwa).

Ibnu Hajar amesema: Na katika istilahi za fani ya Hadithi ni kuwa mpokezi atakaposema; inanasibishwa, Maana yake ni kuwa imevushwa toka kwa Mtume.

(Yaani mlolongo mzima wa wapokezi hadi kumfikia yeye haujatajwa)
Haya yote ni iwapo tutasoma kwa tamko la kutomtaja mtendaji. Ama tukisoma kwa tamko la kumtaja mtendaji, maana yake ni kuwa Sahl ananasibisha hilo kwa Mtume.

Ibnu Hajar ndani ya Fat’hul-Bari  amesema: Ad-Daniyu amezungumzia kuhusu kuvushwa kwa Hadithi hii akasema: Hii ina ila, kwa sababu ni dhana toka kwa Abu Hazimu, na imesemekana kuwa laiti ingekuwa imevushwa basi asingehitajia kusema: “Silijui jambo hili”
Uchambuzi wa hadithi Ya Wailu Bin Hajar:

Muslim amepokea toka kwa Wailu bin Hajar: Kuwa alimuona Mtume kainua mikono yake na kutoa takbira pindi alipoingia kwenye Swala, kisha akajifunika kwa nguo yake, kisha akaweka mkono wake wa kulia juu ya mkono wa kushoto. Alipotaka kurukuu akatoa mikono yake ndani ya nguo kisha akaiinua na kutoa takbira kisha akarukuu…..

Kutumia hoja ya Hadithi hii ni kutumia hoja ya kitendo na kitendo si hoja isipokuwa mpaka ijulikane kwa nini katenda hivyo, na hilo ni jambo lisilojulikana. Kwa sababu dhahiri ya Hadithi inaonyesha kuwa Mtume alikusanya pande za nguo yake akafunikia kifua chake na akaweka mkono wa kulia juu ya mkono wa kushoto.

Je alifanya hivyo kwa kuwa ni jambo la Sunna au alifanya hivyo ili nguo yake isifunuke bali nguo igusane na mwili na kujikinga baridi kwa nguo hiyo?

Anuani ya kitendo haijulikani hivyo kitendo hakiwi hoja mpaka itakapojulikana kuwa alifanya hivyo kwa kuwa ni Sunna ndani ya Sala kufanya hivyo.

Na kuna uwezekano mwingine nao ni kuwa kitendo cha Mtume ilikuwa ni kuzuwia nguo isifunuke ndani ya Sala.

At-Tirmidhiy ametoa toka kwa Abu Huraira kuwa amesema: “Mtume alikataza kufunua nguo ndani ya Sala. Akasema: Kufunua ni mtu kuachia nguo bila kufumba pande za nguo yake mbele yake, hivyo iwapo akiifumba hatokuwa ameifunua, na imepokewa toka kwa Mtume kuwa ni karaha kufunua nguo ndani ya Sala.”

Hakika Mtume aliswali pamoja na Muhajirina na Answari zaidi ya miaka kumi, hivyo laiti kama ingethibiti kufunga mikono toka kwa Mtume basi suala hilo lingenukuliwa kwa wingi na kuenea, na wala asingepokea Wailu peke yake huku katika kunukuu kwake kuna uwezekano wa aina mbili.

Sura Ya Pili Ya Hadithi:
An-Nasai na Al-Bayhaqi wametoa ndani ya vitabu vyao kwa njia mbili tofauti toka kwa Wailu bin Hajar amesema: “Nilimuona Mtume wa Mwenyezi Mungu anapokuwa kasimama ndani ya Swala hufunga mkono wake wa kulia juu ya mkono wa kushoto.”

Katika tamko la Al-Bayhaqi ni: “Anaposimama kwenye Sala hufunga mkono wake wa kushoto kwa mkono wake wa kulia, na nilimuona Al-Qamah anafanya hivyo.”

Kutumia Hadithii kama dalili kunategemea usahihi wa njia ya upokezi na kutimia kwa hoja.

Ama upande wa njia ya upokezi ni kuwa japokuwa mashekhe wawili (Bukhari na Muslim) wameinukuu kwa njia mbili tofauti lakini zote zimeshirikiana kwa kuwepo Abdallah ndani ya njia zote mbili.
Ndani ya Sunan An-Nasai: “Alitupa habari Abdullah”. Ndani ya Sunan Al-Bayhaqi: “Alitupa habari Abdullah bin Jafar” na mkusudiwa ni Abdullahi bin Jafar bin Najihi Al-Saady.
Inatosha kuthibitisha udhaifu wake kwa aliyonukuu Abdallah Ibnu Imam Ahmad toka kwa baba yake: “Wailu alipokuwa akifika kwenye Hadithi yake humtia dosari.”

Sehemu nyingine akasema amenukuu toka kwa baba yake toka kwa mashekhe wake kuwa alisema: “Sikuwa naandika chochote katika Hadithi yake baada ya kunibainikia jambo lake.”
Ad-Dauriyu amesema toka kwa Ibnu Muini kuwa: Si chochote.
Abu Hatim amesema: Yazid ibnu Haruna aliuliza kuhusu yeye, akasema: “Msiulize kuhusu mambo.” Amr bin Ali amesema: “Ni dhaifu.”

Abu Hatimu amesema: Hadithi zake hukanushwa sana, anasimulia toka kwa waaminifu mambo yasiyokubalika. Mpaka akasema: An-Nasai amesema: ‘Hadithi zake huachwa.’ Mara nyingine akasema: “Si mwaminifu.”

Ama hoja ya Hadithi: Kwa sababu huenda Hadithi hii ni picha nyingine ya Hadithi ya kwanza, na tofauti ni kuwa Hadithi ya kwanza ina nyongeza isiyokuwepo kwenye Hadithi hii, kwani katika sura ya kwanza imesemwa kuwa alijifunika nguo yake kisha akaweka mkono
wake wa kulia juu ya mkono wa kushoto.

Tayari imeshapita kuwa dhahiri ya Hadithi ni kuwa Mtume alikusanya pande za nguo zake akajifunikia kifua chake na akaweka mkono wake wa kulia juu ya mkono wa kushoto ili nguo yake isifunuke bali ibakie imegusana na mwili na ajikingie mwili wake dhidi ya baridi.

Hivyo kwa kuwa anuani ya kitendo haijulikani Hadithi hii haiwi hoja kwani haijulikani ni kwa nini alifanya hivyo.
Pamoja na hayo ni kuwa ndani ya Hadithi hii kuna ushahidi unaothibitisha kuwa kitendo cha kufunga mikono hakikuwa kinajulikana kipindi cha mwanzo, kwa sababu ndani ya Hadithi imekuja kauli: “Nilimuona Al-Qamah akifanya hivyo.”
Hivyo laiti kufunga mikono ingekuwa ni jambo lililoenea kati ya maswahaba na waliokuja baada ya maswahaba basi kusingekuwepo na kigezo cha kunasibisha kitendo hiki kilichoenea kwa Al-Qamah mpokezi wa Hadithi toka kwa Wailu.

Na hii inaonyesha kuwa kufunga mkono ilikuwa ni jambo lisiloenea na ndio maana Al- Qamah akalinukuu.

Sura Ya Tatu Ya Hadithi
An-Nasai ametoa kwa njia yake toka kwa Wailu bin Hajar kuwa alisema: Nikasema: Hapana….. Kwenye Sala ya Mtume wa Mwenyezi Mungu jinsi anavyoswali na nikamtazama. Akasimama akatoa takbira na akainua mikono yake mpaka ikalingana na masikio yake, kisha akaweka mkono wake wa kulia juu ya kiganja chake cha kushoto na fundo lake na muundi.

Al-Bayhaqi naye ametoa ndani ya kitabu chake kwa tamko hilo hilo.
Kutumia riwaya hii kama hoja kunategemea usahihi wa njia ya upokezi na hoja yake. Ama kuhusu njia ya upokezi wa An-Nasai, ni kuwa njia hiyo imemjumuisha Aswimu bin Kulaybu Al-Kufiy.
Ibnu Hajar ametaja kuwa alimuuliza Ibnu Shahabu kuhusu dhehebu la Kulaybu je alikuwa Mur’jia. Akasema: Sijui, lakini Shariku bin Abdallah An-Nakhaiy amesema kuwa alikuwa Mur’jia.
Ibnu Al-Madainiy amesema: Hawi hoja akipokea peke yake.

Ama njia ya Al-Bayhaqi yenyewe imemjumuisha Abdallah bin Rajau. Ibnu Hajar amenukuu toka kwa Ibnu Muini kuwa alisema: Alikuwa mwingi wa kukosea maneno, hana ubaya.

Amr bin Adiyu amesema: si mkweli, mwingi wa kuchanganya maneno na kukosea, yeye si hoja, amefariki mwaka 219 au 220 Hijiria.

Ibnu Hajar amenukuu toka kwa As-Sajiy kuwa alisema ana Hadithi zisizokubalika.
Ahmad na Yahya wametofautiana kuhusu yeye. Ahmad amesema:
Wamedai kuwa vitabu vyake vilitoweka hivyo akawa anaandika yale aliyoyahifadhi kichwani, na ana riwaya zisizokubalika, na wala sikusikia toka kwake isipokuwa Hadithi mbili tu. Na maelezo kama haya kaeleza Al-Uqay’liyu toka kwa Ahmad.

Inshallah, kunako majaliwa nitaleta ushahidi wa kuwa Mtume aliswali akiwa amefunga mikono na hadith zilizomadhubuti kuthibitisha hilo.

Namwomba Allah atufanye wepesi wa kuiona haki na kuifuata na pia atufanye kuwa ni wepesi wa kuuona upotofu na kuturuzuku kuuacha.

Comments