MCHANGO WA NASIBA BINT KAAB KATIKA VITA VYA UHUD

MCHANGO WA NASIBA BINT KAAB KATIKA VITA VYA UHUD

Kovu kubwa kwenye mabega ya Nasiba, bintiye Kaab linaashiria kuwepo kwa kidonda kikubwa cha muda uliopita. Wakati wowote wanawake, haswa vijana ambao hawakuiona enzi ya Mtume (s.a.w.w) au walikuwa wadogo wakati huo, walipoliona shimo hilo katika bega lake, waliuliza kwa udadisi mkubwa kuhusu tukio hilo la kutisha ambalo lilisababisha jeraha hilo kwenye bega lake.

Walipenda kusikia kuhusu vituko vyake vya kutisha katika vita vya Uhudi kutoka kwenye mdomo wake mwenyewe.

Nasiba hakudhani angeweza kupigana bega kwa bega pamoja na mumewe na wanawe wawili wa kiume kwa kumlinda Mtume (s.a.w.w) kwenye vita vya Uhudi. Alikuwa amebeba tu kiriba cha maji mgongoni mwake ili awanyweshe majeruhi na pia alikuwa amebeba bandeji za kienyeji kwa ajili ya kuwafunga majeraha yao. Hakuwa amejifikiria kuwa angefaa kwa kazi yoyote nyingine siku hiyo.

Ingawa Waislamu walikuwa wachache na walikuwa na vifaa vichache, waliweza kuwashinda vibaya maadui zao na kuwafanya wakimbie kwenye uwanja wa vita kwa visigino vyao.

Lakini baada ya muda mfupi, kwa sababu ya kutojali na kupuuza kwa walinzi wa “Vilima vya Ainain” maadui walifanya shambulizi la kushitukiza kutoka nyuma yao na kugeuza ushindi wa Waislam kuwa kushindwa. Waislamu waliokuwa wamemzunguka Mtume (s.a.w.w) walikimbia na kumuacha Mtukufu Mtume (s.a.w.w) karibu peke yake kwenye medani ya vita.

Nasiba alipoiona hali hiyo ya hatari mbaya aliweka kiriba cha maji chini, na akachukua upanga mkononi mwake. Alipigana kwa upanga na pia akatumia vizuri upinde na mishale; na akachukua ngao iliyoachwa na mpiganaji anayekimbia.

Mara aligundua kuwa kuna adui ambaye alikuwa akimtafuta Mtume (s.a.w.w), na akiuliza kwa sauti, “Yuko wapi Muhammad mwenyewe?” Alimwendea ghafla na kumpiga mara kadhaa. Lakini yule mtu alikuwa amevaa deraya mbili na hivyo mapigo yake hayakuweza kuwa na athari kubwa mwilini mwake. Kisha akampiga yule mwanamke dhoruba kubwa kwenye bega lake lisilo na deraya na kumjeruhi kiasi ambacho lilihitaji matibabu ya mwaka mzima.

Alipoona damu ikimwagika kutoka kwenye bega la Nasiba, Mtume (s.a.w.w) alimwita mmoja wa watoto wake wa kiume ili amfunge jeraha lake. Alimfunga bandeji kwenye bega lake na akaendelea tena kushughulika na vita.

Wakati huo huo mmoja wa watoto wake akajeruhiwa. Mama yule alitoa bandeji na akamfunga yule kijana kwenye jeraha lake. Mtume (s.a.w.w) akiangalia kitendo hicho na akatabasamu kwa ushujaa na ushupavu wa bibi huyu. Baada ya mama huyo kumhudumia yule kijana alimshauri aendelee na vita. Alipokuwa akiendelea kuzugumza maneno hayo Mtume (s.a.w.w) alimwonyesha yule mtu ambaye alimuumiza na kumjeruhi mwanawe.

Alimshambulia yule mtu kama simba jike na kumpiga upanga wake kwenye mguu mpaka akaanguka chini. Mtume akasema, “Vema, sasa umelipiza kisasi. Sifa njema ni zake Mwenyezi Mungu ambaye amekuwezesha kupata ushindi dhidi yake na kupoza jicho lako.”

Waislamu wengi walikufa mashahidi na wengine kujeruhiwa. Nasiba mwenyewe alikuwa amejeruhiwa sana na hakuwa na matumaini yoyote ya kuishi. Baada ya vita vya Uhud, Mtume (s.a.w.w) aliwaamrisha wale Waislamu waliojeruhiwa kuwafuata maadui mpaka Hamra-ul Asad ili kuhakikisha juu ya nia na hali zao.

Nasiba pia alitaka kuandamana nao lakini yale majeraha makubwa aliyokuwa nayo hayakumruhusu kwenda. Walipokuwa wanarudi kutoka Hamra-ul-Asad, kabla ya Mtume (s.a.w.w) kufika nyumbani kwake, alimtuma mtu kwenda kumjulia hali Nasiba na alifurahi sana kujua kuwa bado alikuwa hai.

Komandoo aliyefanya kazi ya ziada ili kuulinda Ushindi wa waislamu na Uislamu wenyewe ni Imam Ally (a.s) aliyepambana kiasi kwamba waislamu wote walikuwa wamejeruhiwa vibaya na kushindwa kusimama isipokuwa yeye pekee. Vita hii ndio ambayo Mtume aling’olewa meno ya mbele na kudondoshwa ndani ya Shimo na ndipo wengi wa waislamu walidhani amekufa na kumkimbia.

Katika tukio hili sayyidna Hamza (ra) aliuawa na waislamu waliokuwa hawana imani kamilifu kama vile Abubakar na Umar walikimbia mbali sana na kurudi baada ya siku kadhaa.

MAFUNZO KUTOKANA NA HISTORIA HII
1.    Abubakar na Umar hawakuwa na utukufu kama wanavyowatangaza wafuasi wao
2.    Shujaa hasa katika vita hivi ni Mtume na imam Ally
3.    Mwanamke mtukufu Nasiba alikuwa shujaa na bora kuliko wengi wa Masahaba wakiwemo Abubakar na Umar
4.    Kutokumtii Mtume kunaleta maangamizi makubwa kwa Uislamu na waislamu.

5.    Nasiba alikuwa nesi wa kwanza kuwahudumia majeruhi vitani

Comments