MGENI NA MAMA MJANE
Akiwa amechoka na huku amebeba kiriba cha
maji mgongoni, mwanamke alikuwa akielekea nyumbani kwake akiwa mlegevu, na
wanawe wachanga wakiwa wanamsubiri mama mzazi awasili.
Alipokuwa njiani mama huyo alikutana na mgeni
aliyemsaidia kubeba kile kiriba cha maji. Punde si punde waliwasili nyumbani
kwa mama huyo. Baada ya mlango kufunguliwa watoto walimuona mama na mgeni
ambaye aliteremsha kiriba cha maji na akasema:
“Naam, yaonekana kwamba hamna mtu yeyote
wakuwatekea maji! Imekuwaje hadi mkawa na upweke kiasi hiki?”
mama huyo alijibu kwa huzuni: “Mume wangu
alikuwa mwanajeshi; Imam Ali (a.s) alimtuma kwenye mstari wa mbele vitani, na
ndipo alipouwawa. Na hivi sasa nimebaki mpweke na watoto hawa.”
Mgeni huyo alikata kauli na hakuendelea
kuzungumza zaidi. Aliinamisha kichwa chake na akaondoka. Lakini wazo la mjane
na mayatima waliokuwa hawajiwezi halikumtoka.
Na ikawa ndio sababu ya kutolala usiku huo.
Kulipokucha, mgeni huyo alichukua kapu lake, na ndani yake akaweka kipande cha
nyama, unga, na tende. Kisha moja kwa moja alielekea hadi nyumbani kwa mjane
yule na kubisha mlango.
“Ni nani wewe?”
‘’Ni mimi yule bwana aliyekubebea maji jana.
Na hivi sasa nimewaletea watoto chakula.”
“Mwenyezi Mungu (swt) akujaalie kila la kheri
na ahukumu baina yetu sisi na Ali.”
Kisha mama huyo alifungua mlango na kumpokea
bwana huyo. Alipoingia, alitamka na kusema:
“Natamani kutenda mema. Ima uniruhusu nikande
unga na nipike mikate, au uniruhusu niwaangalie watoto.”
“Nashukuru, lakini nadhani nina ujuzi wa
kupika zaidi yako. Wewe waangalie watoto hadi nitakapomaliza upishi.”
Bila kupoteza muda mama huyo alielekea
kukanda unga na bwana huyo alianza kumega nyama aliyoileta na kuwalisha watoto.
Wakati alipokuwa akiweka tonge la chakula mdomoni mwa kila mmoja wao alikuwa
akisema:
“Mwanangu msamehe Ali kama hakuweza
kutekeleza wajibu wake juu yako!”
Unga ulipokuwa tayari kupikwa; mama yule
aliita: “Ewe bwana mungwana washa jiko tafadhali.” Bwana huyo alifanya hivyo.
Moto ulipowaka alisogeza uso wake karibu ya moto na kusema, “Onja joto la
moto.” Hii ndiyo adhabu ya wale walioshindwa kutekeleza wajibu wao kwa mayatima
na wajane.”
Kwa bahati, mwanamke mmoja aliyekuwa jirani
aliingia na baada ya kumtambua mgeni huyo alitiririkwa na machozi. “Ah! Kwani
haumtambui huyu bwana anayekusaidia? Yeye ndiye Amirul Muuminiin ( Kiongozi wa
waumini) Ali bin Abi-Talib (a.s).”
Mjane huyo alisogea mbele huku akilia kwa
kuona haya “Laana na aibu iwe juu yangu. Naomba msamaha wako.”
Hapana, mimi ndiye naomba msamaha kwa
kutotimiza wajibu wangu juu yenu.”
Comments
Post a Comment