MWENENDO WA IMAM SAJJAD (AS)

MWENENDO WA IMAM SAJJAD (AS)

Wakati fulani, mwislamu mwenye kuwachukia Ahlulbayt wa Mtume (s.a.w.w) alimuendea Imam Sajjad (as) na akaanza kumkashifu na kumtukana. Imam (as) hakutamka neno lolote kumjibu lakini, baada ya yule mtu kuondoka kwenye mkusanyiko ule, aliwageukia watu waliokuwepo na kusema:

“Mmesikia aliyosema mtu huyu, sasa ninataka muambatane na mimi mkasikie kile nitakachosema kujibu kashfa na matusi yake”
Masahaba wake wakakubali, “kwa hakika tutaambatana nawe, kwa kusema kweli tulitaraji kuwa ungemjibu wakati ule ule”

Imam (as) aliondoka kuelekea kwenye nyumba ya mtu huyo na alisikika akisoma aya ya Qur’ani ifuatayo:

“Na ambao wanazuia hasira (zao) na wanasamehe (makosa ya) watu; kwani Allah anawapenda wale wafanyao wema (kwa wengine) (Quran 3: 134)

Msimuliaji anasema: “Tuliposikia kisomo cha aya hii, tulijua kwamba Imam (as) alikusudia kuonyesha wema kwa mtu ambaye punde tu alikuwa amemtukana”

Alipofika kwenye nyumba ya mtu huyo, Imam (as) alimuita na akamjulisha kuwasili kwake. Alipomuona Imam, yule mtu akajua kuwa amekuja kujibu kashfa zake.

Lakini, mara tu Imam (as) alipomuona yule mtu, alisema, “Ewe ndugu (yangu)! Ulikuja kwangu na kusema vitu vya kutisha na visivyopendeza.

Ikiwa uliyoyasema juu yangu ni ya kweli, (basi) ninaomba msamaha kwa Allah, lakini ikiwa sio, basi ninamuomba Allah ‘Azza wa Jallah akusamehe.” Yule mtu alishtushwa kusikia maneno haya na akatubu. Alimbusu Imam (as) baina ya macho na akaomba msamaha, akisema:

“Matusi yangu na kashfa hayakuwa na msingi na hayawezi yakahusishwa na tabia yako. Kwa kweli matusi yale yananistahili mimi zaidi kuliko wewe.”

MAFUNZO KUTOKANA NA KISA HIKI:

1.    Matusi dhidi ya Mashia na viongozi wake hayakuanza leo

2.    Wako watu wanadai kuwa ni waislamu lakini hawana adabu kwa Mtume wala Ahlulbayt wake. Watu wa aina hii ni waovu
3.    Wafuasi wa Ahlulbayt wanatakiwa wawe na Subira kama walivyokuwa maimamu watukufu na wawapuuze wale wanaowasingizia kwa kila aina ya uovu.


4.    Waliojijengea tabia ya kukosa adabu na ubabe dhidi ya waislamu wenzao, hawajachelea, muda wao wa kutubu ni huu na watubu sasa kabla hawajaingizwa makaburini. 

Comments