Assalaam alaykum:
Kuna njia nyingi kwa ajili
ya mwanadamu kupata mwongozo na kuibuka kutoka kwenye giza na kuelekea kwenye
nuru. Kwa ajili ya ustawi wa mwanadamu na ukamilifu wa maadili yake, Mwenyezi
Mungu ameumba uthibitisho, ushahidi na dalili1, katika idadi kubwa
kiasi kwamba ziko nje ya uwezo wa kuhesabiwa na kukokotolewa.
Kwa ajili ya mwongozo wa mwanadamu,
Allah aliwatuma mitume na dalili zilizo wazi,2 vitabu, miujiza na
ishara ili pengine watu wanaweza kuitambua njia iliyonyooka na kupata ustawi na
mafanikio.
Katika kipindi chote cha
utume wake, Mtukufu Mtume (saw), katika suala la utakatifu wa kiroho na
ukamilifu wa maadili, alikuwa ni kiigizo katika kauli na matendo, na hata
alisema: “Nimetumwa (kama Mtume) kwa (kusudio la) kuyakamilisha maadili.3”
Tatizo la mwanadamu lipo
katika kutozingatia kwake amali njema, kutenda kwake maovu, kupupia matamanio
na utii kwa shetani. Baadhi ya watu wamejiachia (katika kufanya maovu) kiasi
kwamba wanaendesha maisha yao kama wanyama.
Kwa lengo la utakatifu na
kuyaponya madili ya wanadamu, kupunguza kasi na kudhibiti hulka ya asili,
Mtukufu Mtume alifanya kila aliloliweza na alitaja yote yaliyopaswa juu ya
jambo hili.
Kupata fanaka katika
ulimwengu huu na ulimwengu ujao (Akhera) kunawezekana tu chini ya uangalizi wa
mwalimu na wakati huo huo si kila mtu anaweza kubainisha nukta mbili za mwisho
(yaani maadili bora kabisa na duni kabisa) ili kuonyesha kwa vitendo njia ya
kati na iliyo sawa. Yule mwenye Hikma isiyo na kikomo aliwaleta mitume wote na
hususani Mtukufu Mtume Muhammad (saw) kama “mwalimu na mkufunzi” wa maadili,
ili kwa kufuata nyayo zake, watu wajitenge na maovu na wapate heshima ya duniani
na Akhera.
Katika Qur’ani, kuna sura
iitwayo Al-Qasas (masimulizi), ambayo yenyewe tu ni ushahidi kuwa mwanadamu
anahitaji Historia na masimulizi. Ndio maana sisi Mashia tumezama sana katika
Historia na tunawaomba watu wote wazame katika Historia. Wawatambue watu wema
na kuwafuata na wawatambue pia waovu na kujiepusha nao.
Katika sehemu nyingi ndani
ya Qur’ani, hadithi za mitume wafalme wa mataifa zimetajwa. Kwa kuongezea
Mwenyezi Mungu amezungumzia masuala yanayohusiana na vita, amani, familia,
dini, jamii na mada nyinginezo, katika muundo wa hadithi na masimulizi. Kwa
kuvisoma visa hivi, watu wanaweza kuelewa na kutofautisha kati ya njia ya
maendeleo na ile ya kuporomoka kwa maendeleo, na kupanda na kushuka katika kila
kipengele, hususani maadili.
Suratul Yusuf yote imetumika
kusimulia kisa cha nabii Yusuf, Yaqub, Zulekha na nduguze. Mwanzoni mwa sura
Mwenyezi Mungu anasema:
“Tunakusimulia (Ewe Mtume)
masimulizi bora kabisa kwa (kupitia) yale tuliyokufunulia katika Qur’an hii.
(Suratul Yusuf; 12:13)
Ambapo katika aya ya mwisho
sura hii, anasema katika historia yao, “kwa hakika kuna mazingatio kwa watu
wenye akili.” (Suratul Yusuf 12: 111).
Kwa hakika moja ya ustadi
mkubwa kabisa wa Qur’ani ni hadithi hii ya Yusuf (as) iliyotajwa kuwa ni
“simulizi bora kabisa” na mwisho (Qur’ani) inasema: “katika hadithi hizi kuna
mazingatio kwa wale wanaotaka kuadilika na kufuata njia ya watu watimilifu.
Juu ya hili Amirul Muuminina
(as) katika Nahjul Balaghah, anamuambia mwanawe Imam Hasan (as): “Ingawa
sijafikia umri ule uliofikiwa na wa kabla yangu, nimezitazama tabia zao na
nimetafakari matukio ya maisha yao.
Nilitembea katika maanguko
yao mpaka nikawa miongoni mwao. Kwa kweli, kwa wema wa mambo yao niliyo
(bahatika) kujua, ni kama nimeishi nao mwanzo hadi mwisho.
Hivyo nimeweza kubaini
kilicho kichafu na kisafi na chenye manufaa na chenye madhara.
Nimekuchagulia bora kabisa
ya mambo hayo na nimekukusanyia nukta nzuri huku nikiyaacha yale yasiyo kuwa na
manufaa.”
Narudia kushauri kuwa watu
tusome Historia na hapo ndipo tutaweza kuchagua dini na dini, madhehebu na
madhehebu, mtu na mtu, swahaba na swahaba, imam na imam. Vinginevyo tutabaki
tunafitiniana kwa ushabiki tu.
Na dua yetu ya mwisho (ni)
Sifa zote njema zinamstahiki Allah swt, Mola wa walimwengu.
REJEA
1. Qur’ani Tukufu, Sura
Ibrahim – 14: 5
2. Ibid, Suratul Hadiid
57:25
3. Safinah al-Bihar, Juz
1,uk 411
Comments
Post a Comment