NI LIPI LILILOWAPATA WANAO ?
Baada ya kifo cha imam Ali
(a.s) na Muawiyah kuchukua mamlaka na ukhalifa, alijaribu kulazimisha uhusiano
baina yake na wafuasi (Mashia) halisi wa Ali (a.s). Alifanya jitihada kubwa
kuwataka wafuasi hao wakiri kuwa uhusiano na Ali (a.s) haukuwa na manufaa wala
maslahi yeyote kwao. Bila ya shaka wafuasi hao walipoteza mali na vitu vyao
vingi kwa sababu ya uhusiano huo.
Muawiyah alikuwa na hamu sana
ya kusikia majuto na malalamishi ya hao wafuasi kuhusiana na usuhuba wao na Ali
(a.s), lakini matumaini yake hayo hayakufua dafu.
Wafuasi hao baada ya kifo cha
Ali (a.s) walitambua ubora na utukufu wake zaidi. Vile walivyojitolea muhanga
kwa hali na mali zama za uhai wake, baada ya kifo chake walifanya zaidi ya
hivyo, kwa kumpenda kwa msimamo wake na kwa kudumisha kazi yake.
Wafuasi hao walikabiliana na
misukosuko na kupambana na mitihani kishujaa. Na matokeo yake ni kwamba juhudi
za Muawiyah zilitoa natija tofauti na ile iliyokuwa ikitarajiwa.
Adi mwanae Hatim, aliyekuwa
mkuu wa kabila la Tai ambaye aliheshimika sana baina ya watu wa kabila hilo,
alikuwa ni mtu mwaminifu na mwenye elimu miongoni mwa maswahaba na wafuasi wa
Ali (a.s). Adi, alikuwa na vijana wakiume wengi. Yeye, wanawe na watu wa kabila
lake walikuwa daima tayari kujitoa muhanga kwa ajili ya Ali (a.s). Watoto wake
watatu wa kiume kwa majina ya Tarfa, Turaif, na Tarif waliuwawa katika vita vya
Siffin chini ya bendera ya Ali (a.s). Muda ukapita; Ali akauawa kishahidi;
Muawiya akapora ukhalifa; na Adi siku moja alikutana ana kwa ana na Muawiya.
Ili kufufua zile nyakati zake
za huzuni na kumfanya akiri ni madhara kiasi gani aliyapata katika uhusiano
wake na Ali (a.s). Alimuuliza: “Ni lipi lililowapata vijana wako watatu, Tarfa,
Turaif na Tarif ?”
Adi alijibu: “Waliuwawa wote
kwenye vita vya Siffin chini ya bendera ya Ali (a.s).”
Muawiyah aliendelea, “Ali
hakukutendea haki.” Adi alimuuliza Muawiyah: “Kwa nini?”
“Kwa sababu aliwaelekeza vijana
wako vitani na wake akawahifadhi.” Adi alisema: “ Mimi ndio sikumtendea Ali
(a.s) haki.”
“Kwa nini wasema hivyo?”
“Kwa sababu yeye aliuwawa na
mimi ningali hai. Nilipaswa kujitoa muhanga kwa ajili yake wakati wa uhai
wake.”
Muawiyah alikata tamaa kwa
kuona kuwa hapati kile anachotaka. Na tena kwa upande mwengine alikuwa na hamu
sana ya kusikia kuhusu mienendo na maisha ya Ali (a.s) kutoka kwa wale
walioishi naye kwa muda mrefu.
Basi hapo ndipo ilimbidi
amuombe Adi (a.s) amuelezee juu ya tabia ya Ali (a.s) kama alivyoshuhudia. Adi
aliomba aachwe asizungumze; lakini Muawiyah alisisitiza aongee na hapo Adi
akasema:
“Naapa, Wallahi Ali (a.s)
alikuwa ndiye mtu muona mbali zaidi ya wengine na mwenye nguvu. Alikuwa
akiongea kwa haki, na aliamua kesi kwa uwazi kabisa. Alikuwa ni bahari ya elimu
na hekima. Alikuwa ni mwenye kuchukia fakhari majivuno ya kidunia, na mwenye
kupenda faragha na utulivu wa usiku. Alililia sana kwa ajili ya Allah (s.w.t)
na alikuwa ni mwenye kumfikiria Allah sana.
Katika faragha alijichunguza
nafsi yake mwenyewe na kujisikitikia kwa yale yaliyopita. Alipendelea nguo za
kawaida na kuishi maisha rahisi. Miongoni mwetu alikuwa kama mmoja wetu. Lau
kama tungelitaka chochote kutoka kwake alikuwa ni mwenye kututimizia maombi yetu.
Wakati wowote tulipokuwa tukimtembelea alipendelea tuketi karibu naye bila ya
kuwacha nafasi baina yetu. Mbali na unyenyekevu wote huo, kuwepo kwake kulikuwa
kunatia nidhamu ya woga kiasi kwamba hatukuthubutu kutamka neno kabla yake.
Alikuwa mtukufu kiasi kwamba
hatukuweza kumuangalia. Akitabasamu meno yake yalikuwa yanaonekana kama uzi wa
lulu. “Aliwaheshimu watu waliokuwa waaminifu na wacha-Mungu na alikuwa mkarimu
kwa masikini na wasiojiweza.
Mtu mwenye nguvu hakuwa
anaogopa kutotendewa haki naye wala masikini hawakukatia tamaa uadilifu wake.
Wallahi na naapa, usiku mmoja nilimuona katika sehemu yake ya ibada wakati giza
la usiku lilikuwa limekizingira kila kitu; machozi yakimtiririka usoni na
kwenye ndevu; alikuwa hatulii kama aliyeumwa na nyoka na alikuwa akilia kama
mtu aliyefiwa.”
“Naona kama hata hivi sasa
nasikia sauti yake kama alivyokuwa aki- uhutubia ulimwengu: “ Ewe dunia, wewe ndiye
mwenye kunifuata na kutaka kunihadaa mimi? (Nenda) kamdanganye mtu mwingine.
Muda wako bado haujawadia. Mimi nimekupa talaka tatu ambapo hakuna rejea. Raha
yako haina thamani na umuhimu wako hauna maana. Kwa bahati mbaya! Masurufu ni
machache mno, na safari nayo ni ndefu na pia hakuna swahiba.”
Muawiyah aliposikia maneno
aliyokuwa akitamka Adi, alianza kulia, na baada ya kufuta machozi, alisema:
“Namuomba Mwenyezi Mungu
ambariki Abul Hassan (Ali). Alikuwa kama ulivyomtaja. Sasa niarifu, wajihisi
vipi bila yeye?”
“Najihisi kama mama ambaye
mpendwa wake amechinjiwa mapajani mwake”
“Hutaweza kamwe kumsahau?”
“Hivi dunia itaniruhusu mimi
kumsahau?”
Funzo:
Hivyo ndivyo viongozi hao
wawili walivyokuwa:
1. Muawiyyah,
fitina kwenda mbele na roho mbaya iliyokithiri
2. Imam
Ally uchaMungu na utawa unaoambatana na huruma kwa wanadamu wote.
Comments
Post a Comment