NI LIPI LILILOWAPATA WANAO ?

NI LIPI LILILOWAPATA WANAO ?

Baada ya kifo cha imam Ali (a.s) na Muawiyah kuchukua mamlaka na ukhalifa, alijaribu kulazimisha uhusiano baina yake na wafuasi (Mashia) halisi wa Ali (a.s). Alifanya jitihada kubwa kuwataka wafuasi hao wakiri kuwa uhusiano na Ali (a.s) haukuwa na manufaa wala maslahi yeyote kwao. Bila ya shaka wafuasi hao walipoteza mali na vitu vyao vingi kwa sababu ya uhusiano huo.

Muawiyah alikuwa na hamu sana ya kusikia majuto na malalamishi ya hao wafuasi kuhusiana na usuhuba wao na Ali (a.s), lakini matumaini yake hayo hayakufua dafu.
Wafuasi hao baada ya kifo cha Ali (a.s) walitambua ubora na utukufu wake zaidi. Vile walivyojitolea muhanga kwa hali na mali zama za uhai wake, baada ya kifo chake walifanya zaidi ya hivyo, kwa kumpenda kwa msimamo wake na kwa kudumisha kazi yake.

Wafuasi hao walikabiliana na misukosuko na kupambana na mitihani kishujaa. Na matokeo yake ni kwamba juhudi za Muawiyah zilitoa natija tofauti na ile iliyokuwa ikitarajiwa.

Adi mwanae Hatim, aliyekuwa mkuu wa kabila la Tai ambaye aliheshimika sana baina ya watu wa kabila hilo, alikuwa ni mtu mwaminifu na mwenye elimu miongoni mwa maswahaba na wafuasi wa Ali (a.s). Adi, alikuwa na vijana wakiume wengi. Yeye, wanawe na watu wa kabila lake walikuwa daima tayari kujitoa muhanga kwa ajili ya Ali (a.s). Watoto wake watatu wa kiume kwa majina ya Tarfa, Turaif, na Tarif waliuwawa katika vita vya Siffin chini ya bendera ya Ali (a.s). Muda ukapita; Ali akauawa kishahidi; Muawiya akapora ukhalifa; na Adi siku moja alikutana ana kwa ana na Muawiya.

Ili kufufua zile nyakati zake za huzuni na kumfanya akiri ni madhara kiasi gani aliyapata katika uhusiano wake na Ali (a.s). Alimuuliza: “Ni lipi lililowapata vijana wako watatu, Tarfa, Turaif na Tarif ?”
Adi alijibu: “Waliuwawa wote kwenye vita vya Siffin chini ya bendera ya Ali (a.s).”

Muawiyah aliendelea, “Ali hakukutendea haki.” Adi alimuuliza Muawiyah: “Kwa nini?”
“Kwa sababu aliwaelekeza vijana wako vitani na wake akawahifadhi.” Adi alisema: “ Mimi ndio sikumtendea Ali (a.s) haki.”

“Kwa nini wasema hivyo?”
“Kwa sababu yeye aliuwawa na mimi ningali hai. Nilipaswa kujitoa muhanga kwa ajili yake wakati wa uhai wake.”

Muawiyah alikata tamaa kwa kuona kuwa hapati kile anachotaka. Na tena kwa upande mwengine alikuwa na hamu sana ya kusikia kuhusu mienendo na maisha ya Ali (a.s) kutoka kwa wale walioishi naye kwa muda mrefu.

Basi hapo ndipo ilimbidi amuombe Adi (a.s) amuelezee juu ya tabia ya Ali (a.s) kama alivyoshuhudia. Adi aliomba aachwe asizungumze; lakini Muawiyah alisisitiza aongee na hapo Adi akasema:

“Naapa, Wallahi Ali (a.s) alikuwa ndiye mtu muona mbali zaidi ya wengine na mwenye nguvu. Alikuwa akiongea kwa haki, na aliamua kesi kwa uwazi kabisa. Alikuwa ni bahari ya elimu na hekima. Alikuwa ni mwenye kuchukia fakhari majivuno ya kidunia, na mwenye kupenda faragha na utulivu wa usiku. Alililia sana kwa ajili ya Allah (s.w.t) na alikuwa ni mwenye kumfikiria Allah sana.

Katika faragha alijichunguza nafsi yake mwenyewe na kujisikitikia kwa yale yaliyopita. Alipendelea nguo za kawaida na kuishi maisha rahisi. Miongoni mwetu alikuwa kama mmoja wetu. Lau kama tungelitaka chochote kutoka kwake alikuwa ni mwenye kututimizia maombi yetu. Wakati wowote tulipokuwa tukimtembelea alipendelea tuketi karibu naye bila ya kuwacha nafasi baina yetu. Mbali na unyenyekevu wote huo, kuwepo kwake kulikuwa kunatia nidhamu ya woga kiasi kwamba hatukuthubutu kutamka neno kabla yake.

Alikuwa mtukufu kiasi kwamba hatukuweza kumuangalia. Akitabasamu meno yake yalikuwa yanaonekana kama uzi wa lulu. “Aliwaheshimu watu waliokuwa waaminifu na wacha-Mungu na alikuwa mkarimu kwa masikini na wasiojiweza.

Mtu mwenye nguvu hakuwa anaogopa kutotendewa haki naye wala masikini hawakukatia tamaa uadilifu wake. Wallahi na naapa, usiku mmoja nilimuona katika sehemu yake ya ibada wakati giza la usiku lilikuwa limekizingira kila kitu; machozi yakimtiririka usoni na kwenye ndevu; alikuwa hatulii kama aliyeumwa na nyoka na alikuwa akilia kama mtu aliyefiwa.”

“Naona kama hata hivi sasa nasikia sauti yake kama alivyokuwa aki- uhutubia ulimwengu: “ Ewe dunia, wewe ndiye mwenye kunifuata na kutaka kunihadaa mimi? (Nenda) kamdanganye mtu mwingine. Muda wako bado haujawadia. Mimi nimekupa talaka tatu ambapo hakuna rejea. Raha yako haina thamani na umuhimu wako hauna maana. Kwa bahati mbaya! Masurufu ni machache mno, na safari nayo ni ndefu na pia hakuna swahiba.”

Muawiyah aliposikia maneno aliyokuwa akitamka Adi, alianza kulia, na baada ya kufuta machozi, alisema:
“Namuomba Mwenyezi Mungu ambariki Abul Hassan (Ali). Alikuwa kama ulivyomtaja. Sasa niarifu, wajihisi vipi bila yeye?”

“Najihisi kama mama ambaye mpendwa wake amechinjiwa mapajani mwake”
“Hutaweza kamwe kumsahau?”
“Hivi dunia itaniruhusu mimi kumsahau?”

Funzo:
Hivyo ndivyo viongozi hao wawili walivyokuwa:
1.    Muawiyyah, fitina kwenda mbele na roho mbaya iliyokithiri

2.    Imam Ally uchaMungu na utawa unaoambatana na huruma kwa wanadamu wote.

Comments