SIRI YA MTUMWA MUAMINIFU

SIRI YA MTUMWA MUAMINIFU

Sa’eed Ibn Musayyab anasimulia: “Mwaka mmoja, kulikuwa na njaa kali na hivyo watu walikusanyika pamoja ili kuomba dua kwa ajili ya mvua. Nilitazama hivi na macho yangu yakamuangukia mtumwa mweusi aliyekuwa amejitenga na umati wa watu na akaibukia kwenye kilele cha kilima kidogo.

Nilikwenda katika uelekeo alipokuwa na nilipomkaribia, nilibaini kwamba midomo yake ilikuwa ikijongea (akisoma) dua. Alipomaliza tu dua yake, wingu lilikusanyika angani. Alipoona wingu, mtumwa alimsifu Allah na akaondoka. Mara tu mvua ikatupiga sana mpaka tukafikiri kuwa tunaweza kuangamia. Nilimkimbilia mtumwa yule nikaona kwamba ameingia katika nyumba ya Imam Sajjad (as).

Niliwasili mbele ya Imam (as) na nikasema:
“Ewe bwana wangu! Katika nyumba yako kuna mtumwa mweusi; tafadhali niuzie” Akasema, “Ewe Sa’eed! Kwa nini badala yake nisikupe kama zawadi?”

Na akamuamuru mkuu wa watumwa kuwaleta watumwa wote mbele yake. Walipokuwa wamekusanyika, nilibaini kuwa mtumwa mweusi hakuwa miongoni mwao. Nikasema, “Ninayemtaka hayupo hapa.” Imam (as) akasema hakuna mtumwa aliyebaki isipokuwa mmoja. Kisha akaamuru akaletwe, mtumwa huyo alipoletwa mbele yangu niliona kuwa ndiye mtu mwenyewe niliyekuwa nikimtafuta na hivyo nikasema: “Huyu ndiye ninayemhitaji!”

“Ewe mtumwa! Kuanzia sasa, Sa’eed ni bwana wako na nenda naye” aliagiza Imam (as). Mtumwa akanigeukia na kusema, “Ni nini kilichokusukuma unitenganishe na bwana wangu?” Nikajibu, “Niliposhuhudia dua yako ya mvua ikijibiwa nilitamani kukumiliki.” Aliposikia hivi, mtumwa alinyoosha mikono yake kwa ajili ya dua na akigeuzia uso wake angani akiomba: “Ewe Mola wangu! Hii ilikuwa ni siri baina yangu na wewe. Sasa kwa vile umeivujisha, nipatie kifo na unichukue kwako.”

Imam (as) na wote waliokuwepo walibubujikwa na machozi kutokana na hali ya mtumwa, huku nikitokwa na machozi nilitoka nje ya nyumba. Nilipofika nyumbani kwangu tu, mjumbe wa Imam (as) alifika na kusema, “Njoo kama unataka kushiriki katika mazishi ya sahibu yako.” Nilirudi nyumbani kwa Imam (as) pamoja na yule mjumbe na kukuta mtumwa ameshafariki.

REJEA:
Muntahal Aamal, Juz. 2, uk. 38;

Ithbaat al- Wasiyyah (cha Maasudi)

Comments