WATU WATATU KATIKA PANGO

WATU WATATU KATIKA PANGO

Mtukufu Mtume (saw) amesimulia:
“Watu watatu kutoka katika kabila la Bani Israil walikusanyika na wakaanza safari, walipokuwa njiani, mawingu yalikusanyika na mvua kubwa ikaanza kunyesha na hivyo wakatafuta hifadhi katika pango lililokuwa karibu.

Ghafla jiwe kubwa lilibilingika na kuziba lango la pango, (na hivyo) kuwakwamisha watatu hao ndani na kuubadili mchana kuwa usiku kwa giza. Walikuwa hawana jingine la kufanya isipokuwa kumgeukia Allah kwa msaada.

“Tutumie matendo yetu ya unyofu kama njia ya kupata nusra kutokana na tatizo hili,” alishauri mmoja wao. Wengine wote walikubaliana na ushauri huo. Mmoja wao alisema “Ewe Mola! Unajua kuwa nina binamu yangu anayevutia sana kabisa na kwamba nilivutiwa naye na kumpenda sana, siku moja nilipomkuta akiwa peke yake, nilimchukua na nilitaka kukidhi matamanio yangu ya kimwili, aliposema: ‘Ewe binamu yangu! Muogope Allah na usiuharibu ubikra wangu.’

Niliposikia hivi nilivunjilia mbali matamanio yangu ya kimwili na nikaamua kutofanya kitendo kiovu.

Ewe Mola! Ikiwa kitendo changu hicho kilitokana na unyofu wa kweli na kwa nia ya kupata radhi Zako tu, tunusuru kutokana na huzuni na adhabu. Ghafla waliona kwamba lile jiwe limesogea kidogo, likiruhusu mwanga hafifu kuingia ndani ya pango.
Mtu wa pili alisema: “Ewe Mola! Unajua kwamba nilikuwa na baba na mama, walikuwa wazee sana kiasi kwamba miili yao ilikuwa imepinda kutokana na umri uliopindukia, na kwamba nilikuwa nikiwahudumia kila mara.

Usiku mmoja nikiwa nimewaletea chakula, nilibaini kwamba wote walikuwa wamelala. Nilikesha usiku kucha karibu yao, na chakula mkononi, bila kuwaamsha nikihofia kuwasumbua. Ewe Mola! Ikiwa kitendo changu hiki kilikuwa ni kwa ajili ya kupata radhi na furaha Yako, tufungulie njia na tupe wokovu.” Alipomaliza kauli yake, kundi lile lilibaini kuwa jiwe lile lilikuwa limesogea pembeni zaidi.

Mtu watatu aliomba: “Ewe Mjuzi wa yaliyofichikana na yaliyo dhahiri! Unajua mwenyewe kwamba nilikuwa na mfanyakazi aliyekuwa akinifanyia kazi. Mkataba wake ulipokuwa umefikia mwisho, nilimkabidhi ujira wake, lakini hakuridhika na alitaka zaidi na katika hali ya kutoridhika na kutofurahi, aliondoka.

Nilitumia ujira wake kununulia mbuzi, na niliwahudumia tofauti, na punde nikawa na kundi la mbuzi. Baada ya kipindi fulani, yule mfanyakazi alinijia akitaka ujira wake na nikamuonyesha kundi la mbuzi.

Awali alifikiri ninamdhihaki, lakini baadaye alipotambua umakini wangu alichukua kundi lote (la mbuzi) na kuondoka. Ewe Mola! Ikiwa kitendo hiki kilisukumwa na unyofu na kilikuwa kwa ajili ya kutaka radhi Zako, tuokoe katika mkwamo huu”

Kufikia hapo jiwe lote liliondoka katika lango la pango na wote watatu wakatoka, wakiwa na furaha na msisimko, na wakaendelea na safari yao.

Rejea:
1.    Katika kitabu Mahaasim imetajwa kwamba ujira wake ulikuwa ni nusu dirham lakini alipokuja kuchukua, alipewa mara 18,000 zaidi!
2.    Naamunah-e-ma’arif , Juz.1, uk. 53;
3.    Farajun Ba’d al shiddah, uk 23;

4.    mahaasin e- Barqi, Juz. 2, uk 253

Comments