HOJA YA 2 YA WAPINGA MAULID
Wanadai kuwa Maulidi hayakusomwa na maswahaba wala waandamizi wao (taabi'in). Kama kweli yangelikuwa ni
sawa kuyasoma, bila shaka mabwana wakubwa hao wangelikuwa ni wa mbele kufanya
hivyo.
MAJIBU YETU: Hakuna Mwislamu
yoyote anayekataa kuwa maswahaba ni watu watukufu. Wala hakuna anayekataa kuwa
wao ndio kiungo chetu sisi na Bwana Mtume (s.a.w.w.). Lakini, pamoja na utukufu
wote huo, wao walikuwa ni binadamu; hawakuwa ni ma'asumin. Walikiweza kufanya jambo, wakaswibu (wakapata); kama
ambavyo walikiweza kufanya jambo, wakakosea. Na mifano ya yote mawili hayo ni
mingi katika historia yao.
Kwa hivyo, kuwa tu jambo
fulani halikufanywa na maswahaba, haliwi
ni hoja sahihi ya kuwazuilia Waislamu kulifanya jambo hilo. Hoja ya pekee iliyo
sahihi ni iwapo lile ambalo hawakulifanya wao, waliacha kulifanya kwa sababu
ndivyo alivyoamrisha Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w.), au waliacha
kulifanya kwa sababu linapingana na maamrisho ya Mwenyezi Mungu na Mtume Wake
(s.a.w.w.). Ikiwa walifanya hivyo ndipo jambo hilo litakapokuwa ni hoja; lakini
si kwa sababu ya kuwa halikufanywa na maswahaba, bali ni kwa sababu tu ya kuwa ndivyo alivyoamrisha Mwenyezi Mungu na Mtume
Wake (s.a.w.w.), au ni kwa sababu tu
ya kuwa linapingana na mafunzo ya Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w.) -- na
hivyo ndivyo Kiislamu.
Kwa hivyo si sawa kuyapinga maulidi kwa
sababu tu hayakusomwa na maswahaba na waandamizi wao. La sawa ni kuyapinga kwa sababu tu yamekatazwa na Mwenyezi
Mungu au Mtume Wake (s.a.w.w.), au yanapingana na maamrisho yao. Na hilo, mpaka
hivi sasa, wapinzani wa maulidi hawajaweza kulithubutisha.
Tunasema hivyo kwa sababu, mmoja kati ya misingi muhimu ya sharia ya
Kiislamu, inayokubaliwa na wanazuoni wa wanaosoma maulidi na wale wa wanaopinga
maulidi, ni kwamba -- tunapokuja kwenye mambo kama ya maulidi, ujenzi wa
msikiti, mavazi, na kadhaalika -- kila
kitu ni halali mpaka kithibitishwe kuwa ni haramu. Kwa hivyo, kwa msingi
huu, uharamu wa maulidi haitaki uthibitishwe na wanaoyasoma, bali inataka uthibitishwe
na wanaoyapinga. Wala wasilithibitishe hilo kwa vichwa vyao (Sura 16:116), bali
kwa kutoa ushahidi wa maneno ya Mwenyezi Mungu au Mtume Wake s.a.w.w. (Sura
4:59). Na hilo pia, mpaka dakika hii, wapinzani wa maulidi hawajaweza
kulifanya.
Mwanzo mwanzo wa kuzuka madhihabi haya ya kupinga maulidi, wafuasi wake
waliyapinga mambo mengi yaliyozuka katika zama zao. Kati ya mambo hayo ni
kuvuta sigara, kupiga simu ya waya (telephone),
kujiwekea kashida mbele ya mtu anaposwali, kumwamkia mtu kuwa:
"Umeamkaje?", kupana mikono baada ya swala, kutandika busati
misikitini, na hata kuvaa nguo yenye thamani inayozidi dirhamu 100 (mia)!
Yote hayo waliyapinga kwa hoja ya kuwa hayakuwako zama za Mtume
(s.a.w.w.), na kwamba hayakufanywa na maswahaba na waandamizi wao! Lakini,
baada ya kutambua walikosea wapi, walirudi nyuma, wakayakubali yote hayo. Kwa
maneno mengine, yakawa sio bid'a
tena!
Leo, kwa hoja hizo hizo, waandamizi wao wameanza kusema vibula
vivunjwe! Kesho watasema na minara nayo ivunjwe! Kesho kutwa watasema mimbari
za mbao au za mawe, nazo pia ziondolewe, zirudishwe zile za vigogo vya mtende;
hata vya mnazi havitafaa! Baada ya hapo ni nini kitakachowazuia wasitwambie
tuondoe feni misikitini, turudi kujipepea kwa nguo zetu kama ilivyokuwa zama za
Bwana Mtume (s.a.w.w.)? Au twende hijja kwa ngamia au farasi badala ya ndege?
Au ni lipi litakalowazuia kutuamrisha kuisoma Qur'ani katika ngozi na mbao,
kama ilivyokuwa zama za Bwana Mtume (s.a.w.w.) na maswahaba, badala ya hii
miswahafu mizuri mizuri tuliyonayo?
Ni matumaini yetu kwamba, kama ambavyo watangulizi wao walirudi nyuma
na kuyakubali yale waliyoyafanya ni bid'a
mwanzo, wao nao watafuata nyayo zao, wayaone maulidi, na mengine kama maulidi,
kuwa sio bid'a iliyokatazwa na Mtume
Muhammad (s.a.w.w.). Alhamdulillaah, baadhi yao wameanza kuona hivyo na kufanya
sherehe za mazazi ya Bwana Mtume (s.a.w.w.). Lakini badala ya kuyaita maulidi, huyaita seera (huu ni ujanza wa kitoto wa kubadili jina, kwa kitu kilekile
wakipingacho)!
Comments
Post a Comment