SOKO LA MAGENDO
Waliomtegemea Imam Ja’far Sadiq
(a.s) waliongezeka kwa idadi na matumizi yake pia. Imam huyo aliamua kuwekeza
kiasi cha pesa kwenye biashara ili aweze kutimiza mahitaji yake ya nyumbani
yaliyoongezeka. Aliandaa kiasi cha dirham elfu moja ambazo alimpa mtumwa wake
aliyeitwa “Musadif” akimuelekeza aende Misri akawekeze pesa hizo kwenye
biashara kwa niaba ya Imam.
Musadif alinunua bidhaa ambazo
kwa kawaida hupelekwa Misri, na alijiunga na msafara wa wafanyabiashara ambao
walikuwa wakipeleka bidhaa kama hiyo Misri.
Walipofika karibu na Misri
walikutana na msafara mwingine ukitoka huko. Waliulizana juu ya habari za kila
mmoja wao. Walipokuwa wakizungumza waligundua kuwa bidhaa ambazo Musadif na
wenzake walikuwa wamebeba hazipatikani huko Misri na zilikuwa zinahitajika kwa
wingi. Walifurahi sana kwa bahati yao njema. Kwa hakika hiyo ilikuwa ni bidhaa
inayotumika sana, na watu walilazimika kuinunua kwa bei yeyote.
Wafanyabiashara hao waliposikia
habari hizo njema waliamua kutumia fursa hiyo na wakakubaliana kwa pamoja kuuza
bidhaa hizo kwa faida ya asilimia mia moja.
Walipoingia kwenye mji hali
ilikuwa kama walivyokuwa wameelezwa. Na kulingana na walivyopatana mwanzo,
walianzisha soko la magendo, na hawakuuza bidhaa hiyo chini ya mara mbili ya walivyonunua.
Musadif alirudi Madina na jumla
ya faida ya Dirham elfu moja. Kwa furaha aliyokuwa nayo alimuendea Imam Sadiq
(a.s) na kumkabidhi mifuko miwili, kila mmoja ukiwa na dirham elfu moja. Imam
aliuliza: “ Ni nini hii?’
“Mfuko mmoja unawakilisha pesa
za mtaji wa biashara ulionipa, na huo mwingine (ambao ni sawa na mtaji) ni
faida niliyopata”
“Kwa kweli faida hii ni ya juu
zaidi kuliko tulivyotarajia. Nieleze ni vipi ulivyoweza kupata faida kubwa kama
hii?”.
“Ukweli ni kwamba wakati
tulipopata taarifa karibu na Misri kwamba bidhaa tuliyokuwa tumebeba ilikuwa
adimu huko, inahitajika kwa wingi, tukakubaliana tusiuze chini ya mara mbili ya
bei yake, na tukafanya hivyo.”
“Mungu Wangu Mtukufu! Ulifanya
kazi kama hiyo! Mlikula kiapo cha kuunda soko la magendo miongoni mwa Waislamu?
Mliapia kutouza bidhaa hiyo chini ya mara mbili ya bei uliyonunua nayo? Hapana,
sitaki biashara kama hiyo na wala faida kama hiyo!!
Kisha Imam akichukua mfuko
mmoja, akasema, “Huu ndio mtaji wangu.” Na huo mfuko mwingine hakuugusa kabisa
na akasema yeye hakutaka kuwa na uhusiano wowote nao.
Kisha akasema: “Ewe Musadif! Ni
rahisi kupigana kwa upanga kuliko kuchuma riziki kwa njia ya halali.”
Comments
Post a Comment