KUZALIWA KWA ALI IBN ABI TALIB

KUZALIWA KWA ALI IBN ABI TALIB

Assalaam alaykum:

Imam Ali (a.s) alizaliwa tarehe 13 Rajab ya mwaka wa thelathini wa Tembo (A.D. 600). Binamu yake, Mtume Muhammad (s.a.w.w), alikuwa ana miaka thelathini wakati huo. Wazazi wa Ali walikuwa ni Abu Talib Ibn Abdul Muttalib, na Fatima, binti Asad, wote wa ukoo wa Bani Hashim.

Ali alizaliwa ndani ya Al-Kaaba huko Makka. Mwanahistoria maarufu, Masud, anaandika kwenye ukurasa wa 76 wa juzuu ya 2 ya kitabu chake, Murujudh- Dhahab kwamba moja ya ubora ambao Ali alikuwa nao ulikuwa kwamba alizaliwa ndani ya Nyumba ya Allah (s.w.t.).

 Baadhi ya mabingwa wengine ambao wathibitisha kuzaliwa kwa Ali ndani ya Al-Kaaba, ni :-
1. Muhammad Ibn Talha Shafii katika Matalibul-usul uk 11.
2. Hakim katika Mustadrak, uk. 483, Juz. 111.
3. Al- Umari katika Sharh Ainia uk. 15.
4. Halabi katika Sira, uk. 165, Juz. 1.
5. Sibt Ibnul- Jauzi katika Tadhkira Khawaisil Umma, uk.7.
6. Ibn Sabagh Malik katika Fusuulul Muhimma uk.14
7. Muhammad Ibn Yusuf Shafi’i katika Kifayatut-Talib uk. 261. 8. Shablanji katika Nurul Absar, uk. 76.
9. Ibn Zahra katika Ghiyathul Ikhtisar, uk.97.
10. Edvi katika Nafahatul Qudsia uk. 41.

Miongoni mwa wanahistoria wa kisasa, Abbas Mahmud al-Akkad wa Misri anaandika katika kitabu chake Al-Abqariyat ul-Imam Ali, (Cairo, 1970) kwamba Ali Ibn Abi Talib alizaliwa ndani ya Al-Kaaba.

Mwanahistoria mwingine wa sasa, Mahmud Said at-Tantawi, wa Supreme council of Islamic Affairs (Baraza la juu la Mashauri ya Kiislamu), Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, anaandika katika ukurasa wa 186 wa kitabu chake kiitwacho Min Fadha-il al-Ashrat al- Mubashirina bil- Janna, kilichochapishwa mwaka 1976 na Matab’a al-Ahram at-Tijariyya, Cairo, Misri hivi:- “Rehma za Allah (s.w.t.) ziwe juu ya Ali Ibn Abi Talib. Alizaliwa ndani ya Al-Kaaba. Alishuhudia kuchipuka kwa Uislamu; alishuhudia Da’wa ya Muhammad na alikuwa ni shahidi wa Wahyi (kushuka kwa Qur’an al-Majid). Mara moja tu aliukubali Uislamu ingawa alikuwa bado mtoto, na alipigana maisha yake yote ili kwamba Neno la Mungu liwe juu kabisa.”

Mshairi wa Kiarabu alitunga ubeti ufuatao juu ya kuzaliwa kwa Ali: Yeye (Ali) ndiye yule ambaye ile Nyumba ya Allah (s.w.t.), iligeuzwa kuwa wodi ya wazazi; Na yeye ndiye aliyeyatupa masanamu nje ya Nyumba hiyo; Ali alikuwa mtoto wa kwanza na wa mwisho, daima kuzaliwa ndani ya Al-Kaaba.

Ilikuwa ni desturi ya Waarabu kwamba wakati mtoto anapozaliwa, aliwekwa chini ya miguu ya sanamu au masanamu ya ukoo huo, hivyo kuashiria “kumkabidhi” kwa huyo mungu wa kipagani. Watoto wote wa Kiarabu “walitolewa” kwa masanamu isipokuwa Ali Ibn Abu Talib. Wakati watoto wengine wa Kiarabu walipozaliwa, mmoja wa waabudu sanamu alikuja kuwasalimia na kuwabeba mikononi mwake.

Lakini Ali alipozaliwa, Muhammad, mjumbe wa Allah (s.w.t.) alikuja kwenye eneo la Al-Kaaba kumsalimia. Alimbeba mtoto huyo mikononi mwake, na kumtoa kwenye kumtumikia Allah (s.w.t.).

Mtume lazima awe alikwishajua kwamba yule mtoto aliyekuwa mikononi mwake siku moja atakujakuwa adui asiyeshindika wa wanaoabudu masanamu wote na washirikina na wa miungu yao na miungu ya kike. Wakati Ali alipokua, aling’oa uabudu masanamu na ushirikina kutoka Arabia kwa upanga wake.

Kuzaliwa ndani ya Al-Kaaba kulikuwa ni moja kati ya sifa nyingi ambazo Mungu amezijaalia juu ya Ali. Sifa nyingine aliyokuwa nayo ni kwamba kamwe hakuabudu masanamu. Hii nayo inamfanya awe wa kipekee kwa vile Waarabu wote waliabudu masanamu kwa miaka na miaka kabla ya kukana uabudu masanamu na kuukubali Uislamu. Ni kwa sababu hii ambapo anaitwa, “Karama llahu waj-hahu” (“Ambaye Allah (s.w.t.) ameutukuza uso wake.”).

Uso wake ulitukuzwa hasa na Allah (s.w.t.) kwani ulikuwa ndio uso pekee katika maswahaba ambao kamwe haukuinama mbele ya Sanamu lolote.

Ali alikuwa ndiye mtoto mdogo kabisa katika familia hiyo. Kati ya kaka zake watatu, Talib na Aqil, walikuwa wakubwa kwa miaka kumi zaidi yake.

Kuzaliwa kwa Ali kuliujaza moyo wa nabii furaha isiyo kifani. Mtoto huyu alikuwa ni mtu mmoja “maalum” kwake yeye. Ingawaje Muhammad alikuwa na binamu wengi wengine na walikuwa na watoto wao mwenyewe, na Ali mwenyewe alikuwa na kaka zake wakubwa watatu; lakini hakuonyesha mvuto wowote juu ya yeyote kati yao.

Ali, na Ali peke yake ndiye alikuwa kitovu cha mvuto wake na mapenzi.

Wakati Ali alipokuwa na miaka mitano, Muhammad alimchukua kama mtoto wake wa kupanga, na kuanzia hapo tena hawakutengana tena daima. 

Comments