BIBLIA NENO
LA MUNGU
Miongoni mwa
nguzo za imani ya Kiislam, kuna nguzo hizi mbili, “Kuamini Manabii wa Mwenyezi
Mungu na kuamini Vitabu vya Mwenyezi Mungu.” Manabii kama Musa, Daudi,
Suleimani na Yesu, na wengine waliotajwa katika Biblia wote wanaaminiwa na kuheshimiwa
na kila Mwislamu safi. Haiwezekani kwa muislamu kuwavunjia heshima mitume hawa
au hata mmoja wao.
Waislamu
wote wanaamini ya kuwa Manabii hao wote walipata ufunuo toka kwa Mwenyezi Mungu.
Mara tu itakapothibitishwa ya kwamba ule ufunuo walipata wao wenyewe na
kusimamia kuandikwa kwake Vitabu walipokuwa hai. Waislamu hawatasita kuukubali.
Lakini kwa
bahati mbaya, maneno ya Biblia si yote yaliyofunuliwa na Mwenyezi Mungu kwa mitume
wake. Historia ya Biblia inaonyesha ya kuwa hii Biblia tuliyo nayo iliandikwa
kufuatia masimulizi ya nyakati mbalimbali za karne nyingi, na imefanyiwa
mabadiliko makubwa, mipachiko na machafuo. Yaani mpaka zama hizi, viongozi wa
makanisa hukaa na kuifanyia mabadiliko biblia bila kuona haya yoyote. Kwa
vyovyote iwavyo mabadiliko haya hayawezi kuwakilisha ujumbe wa mwenyezi Mungu
kwa usahihi kama ulivyokusudiwa.
Wataalamu wa
Historia ya Biblia wanatuambia Agano la Kale la Kiebrania limo katika maandiko
yaliyoandikwa yapata karne 5 au 8 baada ya kuondoka Yesu. Lakini hata kabla ya
hapo, kwa sababu kadha wa kadha, ni wazi kwamba michafuo mingi ilifanywa ndani
ya maandiko hayo ya Kiebrania (Encyclopaedia Britanica, Chapa ya II - chini ya
neno Bible). Hili ndiyo hali ya Agano la Kale.
Hebu sasa
tulichunguze Agano Jipya lililoandikwa baadaye na ndiyo maandiko matakatifu ya Wakristo.
Mtaalamu
mashuhuri wa huko Oxford ameandika haya katika kitabu chake “The Story Behind
the Gospel” yaani (Hadithi ya Undani wa Injili). “Jambo la maana ni kukumbuka
ya kuwa hakuna hata Injili moja iliyopata kuandikwa mpaka miaka mingi sana baada
ya kujificha cha Yesu. Kwa ujumla Injili ya Marko ndiyo inayodhaniwa kuwa ya
zamani zaidi. Inakadirwa kuwa iliandikwa mnano 65 A.D. baada ya kuzaliwa Yesu.
Tarehe ya kusulubiwa kwa Yesu inafikiriwa kuwa mwaka 29 au 30 A.D. Hivyo Injili
hii iko kama miaka 35 hivi nyuma ya habari inazozieleza. Injili zilizobaki ziliandikwa
miaka mingi baadaye.
“Katika
miaka ya mwanzo iliyofuatia kifo cha Yesu hapakuwepo na maandiko yoyote juu ya
maisha na mafundisho ya Yesu. Pengine baadhi ya methali zake mashuhuri zilikuwa
zimeingizwa katika ibara fulani fulani. Lakini kadri miaka ilivyozidi kupita na
maneno ya Yesu kuzidi kusahaulika ilionelewa heri kuyaandika.
Usahihi wa
maandiko hayo awali ulikuwa ni lazima utegemee maoni ya wale walioweza kukumbuka
maneno ya Yesu, kama ilivyokuwa zama zile, na pia masimulizi ya wale waliokua
na Yesu na kumsikia, na Injili za leo zimeandikwa kufuatia visa na masimulizi
haya.
Ukweli ni
kuwa habari, hata ikiwa ni juu ya jambo lililotendeka hivi punde tu, ni vigumu
sana kupita kinywa hata kinywa bila ya kupata mabadiliko. Hivyo linakuwa ni
jambo lisilopingika ya kwamba masimulizi ya Yesu yalivyopitia kinywa hiki hadi
kile kwa muda wa miaka thelathini (katika zama za giza) yalipata mabadiliko
makubwa katika muda huo wote.
Kadhalika yatupasa
tukumbuke ile desturi ya waandishi wa kale, kwani wao walipoandika habari za
mtu fulani walitumia maneno waliyoona yanatimiza mradi wao bila ya kukusudia
kudokeza ya kuwa hayo ni sahihi na ni yale yale aliyoyatamka yule mtu mwenyewe.
Wala hapakuwa na mwandishi wa kale aliyekuwa mwangalifu hivi kwamba
aliyachungua na kuyakariri maandiko yake hata yakaweza kufafanua mradi kamili
wa jambo alilokusudia kueleza.
Bila shaka
Injili, ambazo hazikuandikwa kama kumbukumbu tu bali kama mafundisho pia,
zilihusikana sana na tabia hii ya mwandishi wa kale. Kwa hivyo hatuna usalama
wowote ya kuwa visa na methali kama tusomavyo katika Biblia zinawakilisha
matendo hasa yaliyotendeka na maneno ya asili yaliyonenwa,” (The Story Behind the
Bible, by Mr. Allen, ukurasa 44).
Kwa maana
hii, Biblia ni hati iliyoandikwa na watu kufuatia mila na methali iliyorithiwa
toka kizazi hata kizazi. Karne nyingi zilipita kabla Biblia haijaingia katika sura
yake ya hivi sasa, na katika muda huo mrefu, ilifanyiwa mabadiliko mengi,
mipachiko na machafuo chungu nzima. Katika hali hii Biblia kimekuwa kitabu
kinachokusanya ukweli uliochanganyika na uzushi, upungufu na maneno
yasiyopatana.
Baadhi ya
ukweli uliomo Bibliani, ni bishara ambazo katika hizo nyingi zilitimia kwa
kufika kwake Mtume Muhammad (s.a.w.w), kunako majaliwa ya Allah, nitazieleza
taratibu tena kwa umakini mkubwa.
Kuja kwa
Nabii Muhammad (s.a.w.w) si jambo geni kwa watu wa kitabu maana kumebashiriwa
mara nyingi katika Biblia. Haya yanathibitishwa na Qur’an Tukufu inayosema hivi
juu ya waaminio kwamba ni wale “Ambao wanamfuata Mtume, Nabii aliye Ummi, ambaye
wao humkuta ameandikwa kwao katika Taurati na Injili. Huwaamuru yaliyo mema na
kuwakataza yaliyo mabaya.” (7:158).
Maneno haya
“Ameandikwa kwao katika Taurati na Injili”, yanaonyesha kwamba Nabii Muhammad (s.a.w.w)
si Mtume wa kitaifa bali ametumwa kwa mataifa yote ya wanadamu. Yeye ni mbora
wa mitume wote (Sura 33:41) naye alitumwa kwa watu wote (Sura 7:159) bishara zinazotabiri
kuja kwake zinapatikana katika vitabu vya dini zote. Hapa vimetajwa Taurati na
Injili. Katika vitabu hivyo mna bishara nyingi zenye kuwawezesha Mayahudi na
Wakristo kumtambua Mtume Muhammad (s.a.w.w).
Comments
Post a Comment