HADITH YA KARATASI
Hii ni Hadith iliyo mashuhuri
sana. Wanazuoni wa Hadith wameitaja
katika vitabu vyao, na vile vile wanahistoria kadha wa kadha wameitaja katika
vitabu vyao. Na kati ya wote hao hakuna hata mmoja aliyekikanusha kisa hicho,
wala kukitilia shaka.
Kati ya vitabu vya Hadith
vilivyosimulia kisa hiki ni Sahih Bukhari. Kwa masunni, hiki ndicho kitabu
kilicho sahihi mno, na kwa hivyo kuaminiwa mno, baada ya Qur’ani Tukufu. Katika
kitabu hicho mna riwaya saba zinazosimulia kisa hicho. Kwa faida ya wasomaji wetu, hapa chini tunazidondoa zote:
1. Imepokewa
kwa Ibn Abbas akisema: “Mtume (s.a.w.w.)
alipozidiwa na maradhi yake, alisema: Nileteeni (karatasi ya) kuandikia, niwaandikie maneno ambayo
baada yake hamutapotea. Lakini Umar akasema:
Hakika Mtume (s.a.w.w.) amezidiwa na maradhi, na sisi tunacho Kitabu cha
Mwenyezi Mungu. Kinatutosha. Hapo basi (maswahaba) wakakhitalifiana, na zogo likazidi, (Mtume s.a.w.w.) akasema:
Niondokeeni! Haifai kuzozana mbele
yangu.”
Ibn Abbas akatoka huku anasema:
“Msiba ulioje wa Mtume (s.a.w.w.) kuzuiwa kuandika (alichotaka kuandika).”
Hadith hii imo katika Kitaabul
Ilm, Mlango wa Kitaabatil Ilm. Kwa tafsiri ya Kiingereza ya kitabu hicho, ni
Hadith Na. 114, uk. 86 wa Juzuu ya Kwanza.
2. Imepokewa
kwa Said bin Jubayr kwamba alimsikia Ibn Abbas r.a. akisema: “Siku ya Alkhamisi!
Na ni ipi hiyo siku ya Alkhamisi?” Kisha
akalia mpaka mawe yakaroa kwa machozi
yake.
Nikamuuliza:
“Ewe Ibn Abbas! Ina nini hiyo siku ya Alkhamisi?” Akasema: Mtume wa Mwenyezi
Mungu (s.a.w.w.) alizidiwa na maradhi yake. Akasema: Nileteeni mfupa wa bega
niwaandikieni maneno ambayo baada yake hamutapotea abadan. (Maswahaba) hapo wakazozana, wala
haifai kuzozana mbele ya Mtume s.a.w.w.
Na wakauliza: Ana nini? Anaweweseka?
Muulizeni (ili mujue hali yake). Yeye s.a.w.w.
akasema: Niacheni! Niliyonayo ni bora kuliko hayo munayonitaka nyinyi niyafanye.
“Hapo (Mtume s.a.w.w.)
akawaamrisha mambo matatu. Akasema: Watoeni Bara Arabu washirikina wote, wapeni
zawadi wajumbe (wa kigeni wanapokuja kwenu) kama nilivyokuwa nikiwapa mimi.
Msimuliaji akaongeza: “La tatu ni jambo la kheri ambalo ama Ibn Abbas
alilinyamaza, au alilitaja lakini nimelisahau!”
Hadith hii imo katika Kitaabu
Fardhil Khumsi, Mlango wa Ikhraajil Yahudi Min Jaziratil Arab. Kwa Kiingereza
ni Hadith No. 393, uk. 260 wa Juzuu ya Nne.
3. Maneno
ya hii Hadith ya tatu karibu yote ni sawa na yale ya Hadith Na. 2 hapo juu.
Nayo imo katika Kitaabul Maghaazil, Mlango wa Maradhin Nabiyyi (s.a.w.w.) wa
Wafaatihii. Kwa Kiingereza, ni Hadith Na. 716, uk. 511 wa Juzuu yo Tano.
4. Imepokewa kwa Ubaydullah
kwamba Ibn Abbas r.a. amesema: “Mtume wa
Mwenyezi Mungu (s.a.w.w.) alipouguwa maradhi ambayo ndiyo aliyofia, na nyumbani
mwake mkawa muna watu akiwamo Umar miongoni mwao, alisema: Njooni niwaandikie
maneno ambayo hamutapotea baada yake. Umar akasema: Hakika Mtume s.a.w.w.
amezidiwa na maradhi, na nyinyi munayo
Qur’ani. Kinatutosha Kitabu cha Mwenyezi
Mungu. Watu waliokuwapo hapo nyumbani wakazozana.
Wengine walisema: Njooni karibu
ili Mtume (s.a.w.w.) atuandikie maneno
ambayo hatutapotea baada yake. Na wengine wakasema alivyosema Umar.
Walipozidisha zogo lao na ikhtilafu zao mbele ya Mtume (s.a.w.w.), Mtume
wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w.) alisema:
Niondokeeni!
“Ubaydullah anasema: Ibn Abbas
alikuwa akisema: Msiba ulioje wa Mtume
wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w.) kuzuiwa kuyaandika
maneno haya kwa sababu ya ikhtilafu zao na zogo lao.”
Hadith hii imo katika Kitaabul
Mardhwaa, Mlango wa Qawlil Mariidhwi
Quumuu Annii. Kwa Kiingereza ni Hadith Na. 573,
ukurasa wa 389 wa Juzuu ya Saba.
4. Maneno
ya hii Hadith ya tano karibu yote ni sawa na yale ya Hadith Na. 4 hapo juu.
Nayo imo katika Kitaabul
I’tiswaami Bil Kitaabi was Sunnah, Mlango wa Karaahiyatil Ikhtilaaf. Kwa Kiingereza
ni Hadith Na. 468, ukurasa wa 346 - 347 wa Juzuu ya Tisa.
Kitabu kingine kinachosimulia
Hadith hii ni Sahih Muslim. Kitabu hiki,
kwa masunni, ndicho cha pili (baada ya Sahih Bukhari) kilicho sahihi mno baada
ya Qur’ani Tukufu. Maneno ya Hadith
iliyomo humu ni karibu sawa na yale yaliyonukuliwa na Bukhari katika
Hadith Na. 2 hapo juu.
Hapa ningependa tukumbushane
wanavyosema wanazuoni wa kisunni wa fani
ya Hadith. Wao wanasema: Iwapo Hadith imepokewa na Bukhari na Muslim (wote
wawili pamoja), basi Hadith hiyo
huhisabiwa kuwa i sahihi mno (mu’tafaq alayhi). Ya pili kwa usahihi ni ile
iliyopokewa na Bukhari peke yake. Ya tatu ni ile ya Muslim pekee.
Comments
Post a Comment