MAELEZO YA MASHIA KUHUSU MWANZO WA WAHYI

MAELEZO YA MASHIA KUHUSU MWANZO WA WAHYI

Assalaam alaykum:

Waislamu wa Shia, wanaamini kuwa mtume Muhammad Mustafa (s.a.w.w), alipofikia na malaika Jibril siku aliyomtokea kwa mara ya kwanza, alimkaribisha kama aliyekuwa akimtarajia. Jibril alimletea zile habari njema kwamba Allah (s.w.t.) amemchagua yeye kuwa Mtume Wake wa mwisho kwa wanadamu na akampongeza kwa kuteuliwa kuwa mpokeaji wa heshima kubwa kuliko zote kwa mwanadamu katika dunia hii.

Mtume Muhammad (s.a.w.w) hakusita katika kuupokea ujumbe wa Utume wala hakuwa na ugumu wowote katika kurudia zile Aya za Wahyi wa mwanzo. Alizisoma au kuzirudia bila ya taabu yoyote, mwenyewe. Jibril, kwa kweli, hakuwa mgeni kwake, na alijua pia kwamba sababu ya kuwepo kwake mwenyewe ilikuwa ni kutekeleza ujumbe uliowekwa juu yake na Allah (s.w.t.) kama Mtume Wake. Alikuwa “mwenye kuuelewa ujumbe” hata kabla ya kufika kwa Jibril.

Waislamu wa Shia pia wanasema kwamba kitu kimoja ambacho Jibril hakuwa akifanye, kilikuwa ni kutumia nguvu za kimwili juu ya Mtume kusoma. Kama alifanya, itakuwa kwa kweli ni mtindo wa ajabu wa kumpa mtume Muhammad (s.a.w.w) huo uwezo wa kusoma – kwa kumminya au kumkaba. Wanasisitiza zaidi kwamba Mtume hakuazimia kujiuwa katika wakati wowote wa maisha yake, sio hata katika nyakati za huzuni sana; na kwamba haijawahi kumjia kwamba angeweza kamwe kuguswa na “uovu” au kwamba angeweza “kupotoshwa” au “kuchafuliwa.”

Hata hivyo, Mtume alihisi wasiwasi juu ya ukubwa wa jukumu lililo mbele yake. Alitambua kwamba katika utekelezaji wa kazi yake, atakuja kukabiliwa na upinzani mkubwa, mgumu, na uliodhamiriwa wa mapagani wa dunia nzima. Ile hali ya wasiwasi wake ilikuwa karibu kudhihirika.

Alikuwa, kwa hiyo, kwenye hali ya uzito wa mawazo alipoondoka pale pangoni kurudi nyumbani. Na alimuomba Khadija kumfunika ndani ya blanketi wakati akikaa chini kumuelezea yale matukio ya kule Hira.

Khadija alipoisikia Hadith aliyomwambia Mtume, alimliwaza na kumpa moyo kwa kusema, “Ewe mwana wa ami yangu, kuwa mwenye furaha nzuri, Allah (s.w.t.) amekuchagua wewe kuwa Mtume Wake. Wewe siku zote ni mpole kwa majirani zako, mwenye msaada kwa jamaa zako, mkarimu kwa mayatima, wajane na masikini, na mwenye upendo kwa wageni. Allah (s.w.t.) kamwe hatakuacha wewe peke yako.”


Inawezekana kwamba Muhammad alizidiwa kwa muda kidogo na mawazo juu ya uwajibikaji wake kwa Allah (s.w.t.) katika kuubeba mzigo mzito wa jukumu lake jipya, lakini pale aliposikia maneno ya kuliwaza ya Khadija (mama wa waumini), mara moja alijisikia zile fadhaa zote ndani yake zikipungua. Alimtuliza na kumpa moyo kwamba pamoja na Mkono wa Allah (s.w.t.) juu ya bega lake, atasimama sawia na majukumu yake na ataweza kushinda vikwazo vyote. 

Comments