UTABIRI WA TANO WA MTUME MUHAMMAD (S.A.W.W) NDANI YA BIBLIA.
Katika Isaya
(21.13-17) mmeandikwa: “Hili ni neno zito lililo juu ya Arabia. Ninyi mtalala
ndani ya msitu wa Arabuni, enyi Wadedani wenye kusafiri pamoja, Wenyeji wa nchi
ya Tema walimletea maji yule aliyekuwa na kiu, walimlisha mkate wao yule
aliyekimbia.
“Kwani
walizikimbia hizo panga, huo upanga uliofutwa, na huo uta uliopindwa, na hayo
mazito ya vita. Kwani yeye Jehova ameniambia neno hili, katika muda wa mwaka
mmoja, kwa kuandama hesabu ya miaka ya mwenye kuajiriwa, huo utukufu wote wa
Kedari utabatilika, na hao watakaosalia katika hesabu ya hao wenye kutumia uta,
hao Mashujaa wa hao wana wa Kedari, watakuwa ni wachache kwa maana Jehova, yeye
Mwenyezi Mungu wa Israeli, amenena neno hili.”
1. Aya 13 inatabiri juu ya “Hijra”
yaani kuhama kwa Mtume Muhammad (s.a.w.) kutoka Makka hadi Madina. Tukio hili
ni mojawapo katika matukio matukufu sana katika historia ya dini ya Kiislamu,
maana Kalenda ya Kiislamu huanzia tangu wakati huo. Mtume s.a.w. alipotoka
Makka kwa amri ya Mwenyezi Mungu na kuhamia Madina ambako alistawi sana na
baadaye akiwa na masahaba wake watakatifu elfu kumi alirudi kuingia Makka bila kizuizi.
2. Maneno ya Aya 14 yanaeleza hali
ya Mtume (s.a.w.) aliposafiri kuhamia Madina. Ikumbukwe ya kwamba Tema ndilo jina
la nchi ambamo miji ya Makka na Madina yapatikana.
3. Maelezo ya aya 15, ni juu ya ile
hali ya nchi yenye mateso na usumbufu juu ya Mtume (s.a.w.) ambayo watu wa
Makka walimtendea hata maisha yake yakawa katika hatari katika mji huo
alimozaliwa. Katika kitabu cha Maisha ya Mtume Muhammad, kilichoandikwa na
marehemu Al-Haj F. R. Hakeem uk. 22 imesimuliwa hivi :-
“Mwisho saa ilifika. Wakimkuta
Mtume (s.a.w.) akielekea kuwa peke yake kabisa, Wakubwa wa Kikureshi walifanya
mkutano katika Dar-un-Nadwa.. ambako mambo ya kiserikali yalifikiriwa na
mashauri kukatwa. Walikutana huko na kushauriana jambo gani afanyiwe. Baadhi
yao walifikiri afungwe kamba na atupwe katika chumba cha giza na aachwe bila
chakula mpaka afe.
Wengine walifikiri asafirishwe
mbali sana. Lakini, mwishowe Abu Jahli aliwapa mawazo yake ya kwamba vijana wa
ukoo mkuu wapewe panga kali, ambao watatumia kwa kumhujumu kwamba wote
watamshambulia wakati mmoja ili pasiwe na kabila maalumu la Makureshi la
kushtakiwa kwa kuua. Bani Hashim (Kabila la Mtume, s.a.w.) lingeridhika, kwa
hivyo kupewa pesa za damu badala ya kuwaadhibu.
“Mpango huu ulikubaliwa na watu
wote. Baadaye watu walio na silaha walijipanga nje ya nyumba ya Mtume (s.a.w.)
tayari kumuua akitoka nje. Lakini Mwenyezi Mungu alimwepusha na hila zao mbaya
na akamwepusha na panga zao zilizokuwa kali.”
Hii ndiyo iliyokuwa hali ya mji
wa Makka Mtume alipouhama, na hizi hasa ndizo hali zilizotabiriwa na maneno
hayo ya Isaya.
4. Aya 16 yatabiri juu ya vita vya
Badr, ambavyo Mtume (s.a.w.) na wafuasi wake wachache walipigana na kundi kubwa
la maadui wa Uislamu mwaka mmoja baada ya Mtume kuhamia Madina.
Katika vita hivi vilivyopiganwa
karibu na mji wa Madina, Waislamu wachache waliokuwa na silaha haba
waliwashinda maadui zao waliokuwa wengi sana tena mahodari wa vita.
Hesabu ya Waislamu ilikuwa 313
hali maadui zao walikuwa elfu moja. Lakini kwa kudra ya Mwenyezi Mungu, mwenye
uwezo wote, maadui wa Uislamu walishindwa vibaya sana na utabiri uliyotajwa
hapo juu ukatimia barabara.
Pia ikumbukwe ya kwamba Kedar ni
jina la mtoto mmoja wa Ismaili ambaye wazao wake waliishi katika sehemu ya
Hijaz ulipo mji wa Makka. Wataalamu wa historia wamethibitisha kuwa Makureshi
wa Makka (ambao ndio wale waliopeleka jeshi Madina kwenda kuwasaga Waislamu,
lakini badala yake wakasagwa wao) walitokana na hao wazao wa Kedar. Na kule
kushindwa kwao baada ya mwaka mmoja baada ya Mtume (s.a.w.) kuhamia Madina kunakamilisha
utabiri huu wa Isaya bila upungufu wo wote.
5. Ile aya ya mwisho, yaani 17,
inatabiri ushindi wa Mtume (s.a.w.) juu ya maadui zake katika hivyo vita
vilivyotokea mwaka mmoja baada ya Mtume kuhamia Madina. Kwa jumla utabiri huu mzima
hauna uhusiano wo wote na Nabii mwingine ila tu Nabii Muhammad (s.a.w.) Wala
hapana ushahidi wa historia unaoweza kutufanya tuseme ya kwamba pana Mtume mwingine
aliyehama mji wake kwa ajili ya maadui zake na kisha akawashinda hao hao baada
ya mwaka mmoja. Hayo yote yalitokea kwa Mtume wetu mtukufu Muhammad (s.a. w.)
pekee.
Comments
Post a Comment