UCHAMBUZI WA HOTUBA YA SHEIKH UWESU KATIKA MAZISHI YA DOCTOR KABOUR.


UCHAMBUZI  WA HOTUBA YA SHEIKH UWESU KATIKA MAZISHI YA DOCTOR KABOUR.

Wiki hii tulimpoteza kiongozi maarufu wa mkoa wa Kigoma, na Tanzania kwa ujumla, hususan kwa upande wa CHADEMA NA C.C.M.
Dr Kabour alikuwa mbunge wa kwanza wa upinzani Tanzania nzima kuingia bungeni kwa tiketi ya chama cha upinzani (CHADEMA). Yeye aliingia bungeni kabla ya uchaguzi mkuu uliohusisha vyama vingi vya siasa mwaka 1995. Hii ilitokana na uchaguzi mdogo uliofanyika Manispaa ya kigoma Ujiji baada ya kumpoteza mbunge wake wa kipindi hicho, marehemu Rajabu Mbano.
Dr. Kabour aliwahi kuwa makamu mwenyekiti wa CHADEMA taifa,  mbunge wa Afrika na mwenyekiti wa CCM wa mkoa wa Kigoma. Alifariki wiki hii alipokuwa akipatiwa matibabu katika hospitali ya taifa Muhimbili na kusafirishwa hadi kigoma na kuzikwa Ujiji siku ya Ijumaa iliyopita.
Tunamwomba Allah amsamehe, na kumwingiza katika rehema zake. (Sote tuitike Ameen).

Sheikh Uwezo Khalifan Kiumbe anasema, kumekuwepo na mijadala katika vijiwe, hususani vya kahawa kujadili uhalali wa sisi kumsafirisha Marehemu Kabour kutoka Dar Es Salaam mpaka Kigoma umbali wa zaidi ya kilometa elfu moja, wakati Mtume alituagiza Mtu azikwe mahali alipofia.

Akilitetea tendo lao hilo anasema kuwa walimsafirisha marehemu kwa sababu huo ndio ulikuwa wosia wake, yaani azikwe Ujiji, na kaburi lake lijengewe baada ya siku saba tokea kuzikwa.

Akaendelea kusema kuwa katika Uislamu wosia ni muhimu uzingatiwe. Na hilo sio geni kutekeleza wosia ulioachwa na Marehemu. Kisha akatoa mfano wa wosia waliowahi kuutekelezwa na masahaba wa Mtume (s.a.w).

Akasema kuwa Bibi Fatuma bint Rasulillah (s.a.w) alikufa akiwa hawaridhii mabwana wawili Abubakar na Omar. Fatuma ndio mtoto pekee aliyeachwa na Mtume pindi alipofariki. Ieleweke kuwa Mtume anasema kuwa Fatuma (a.s) ni mwanamke wa kwanza kuingia peponi. Hivyo jambo alilofanya haliwezi kuwa nje ya Uislamu.

Baada ya baba yake (Mtume) kufariki, na Abubakar kuchukua ukhalifa, alikwenda kwa Abubakar kudai mirathi yake. Abubakar akadai kuwa alimsikia Mtume akisema kuwa mitume hawarithiwi. Ikabidi Fatuma akose mirathi yake na hapo akamchukia sana Abubakar.

Siku chache baadaye bibi huyu akafariki na kuacha wosia kuwa mabwana wawili Abubakar na Umar wasihudhurie mazishi yake. Hili lilitekelezwa na mabwana hao hawakuhudhuria mazishi yake. Huu ni mfano wa utekelezaji wa wosia wa marehemu tena uliofanywa na watu wema.

Kwa bahati mbaya hakueleza sababu za bibi huyu mtukufu kumchukia Omar. Lakini kwa wachunguzi wa mambo wanafahamu. Ukweli ni kuwa ukhalifa wa Abubakar ulitokana na Omar kuwalazimisha watu wamtii Abubakar, kiasi kwamba alikwenda nyumbani kwa bibi huyu mara nyingi na kuwalazimisha waislamu waliokuwa wakijua kuwa khalifa wa kwanza ni imam Ally (a.s) wabadili misimamo na hivyo kumtii Abubakar kama khalifa wa kwanza.

Katika pilika pilika hizi, alifikia mahala kupiga ngumi mlango wa bibi huyu na yeye akiwa nyuma yake, hapo mlango ukampiga tumboni na kupelekea kupoteza ujauzito aliokuwa nao, ndipo akaugulia kipigo hiki na miezi miwili baadaye akafariki dunia. Hivyo alimchukia Omar kwa sababu ndiye aliyekuwa sababu ya kifo chake.

Ikumbukwe kuwa Uwesu huyu ndiye yule yule aliyesimama majukwaani na kudai kuwa mashia ni makafiri. Tulipomuuliza ukafiri wetu akasema kuwa tunawatukana maswahaba. Tulipomwambia tukisemacho ni historia iliyomo katika vitabu vya Ahlul Sunnah alidai kuwa ni mashia ndio waliozipachika historia hizo katika vitabu vyao.  
Lakini leo anakuja na maelezo yale yale ambayo yanaponukuliwa na Mashia, wao huchachamaa na kudai kuwa mashia wanawatukana masahaba.

Hoja zangu ni hizi:
1.    Nani alikuwa kwenye haki kati ya bibi Fatuma na Abubakar katika suala la mirathi?
2.  Je mtu mtakatifu kama Fatuma anaweza kwenda kudai mali zisizokuwa halali yake? Na bado awe mtu wa peponi?
3.  Qur’an inasema kila mtu anarithiwa, je mitume hawakuwa watu?
4.  Qur’an inasema kuwa Seleman alimrithi Daudi, je Daudi hakuwa mtume? Mbona alirithiwa na Seleman?
5.  Je aliyedhulumu na aliyedhulumiwa, wote kwa pamoja wamo katika haki? Fikiri kiundani.
6.  Wakati akitutukana mashia kwamba hoja zetu zinawatukana maswahaba, je Uwesu hakuwa amevisoma vitabu vya historia na kuuona ukweli huo? Je sasa ndio ameuona ukweli? Kama ameujua ukweli hatutegemea achukie pale tutakapo hadithia historia za masahaba waovu na madhalimu.

7.   Au alikuwa akiujua lakini alikuwa akiuficha ukweli? Kama alikuwa akiuficha ukweli basi atakuwa ni mnafiki na wafuasi wake pia ni wanafiki.

Comments